Kikosi cha Dodoma Jiji FC kimeibuka na ushindi mkubwa wa mabao 3-2 dhidi ya mabingwa watetezi Young Africans SC katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliopigwa leo Mei 13, 2026 kwenye Uwanja wa Airtel, Singida.
Huo umekuwa mchezo wa kwanza kwa Yanga kupoteza msimu huu wa ligi baada ya kucheza mechi 22 bila kufungwa, jambo lililoongeza presha katika mbio za ubingwa wa ligi hiyo.
Ushindi huo umeifanya Dodoma Jiji kupanda hadi nafasi ya saba kwenye msimamo wa ligi kwa kufikisha pointi 32, ikiishusha Pamba Jiji FC kutoka nafasi hiyo, huku zikiwa zimesalia mechi saba kabla ya msimu kumalizika.
Yanga ilianza mchezo kwa kasi na kufanikiwa kupata mabao mawili kupitia kiungo wake mahiri Allan Okello ambaye aliendelea kuonyesha kiwango bora msimu huu.
Hata hivyo, mambo yalianza kubadilika dakika ya 28 baada ya nahodha wa Yanga Bakari Mwamnyeto kujifunga wakati akijaribu kuondoa krosi ya William Edgar na kuipa Dodoma Jiji bao la kwanza.
Bao hilo lilionekana kuathiri utulivu wa kipa wa Yanga Djigui Diarra ambaye alipoteza nafasi ya kuandika clean sheet nyingine dhidi ya Dodoma Jiji.
Diarra alitolewa dakika ya 38 kutokana na maumivu na nafasi yake kuchukuliwa na Hussein Masalanga, huku kipa huyo raia wa Mali akionekana kutoridhishwa alipokuwa akielekea benchi.
Kipindi cha pili Dodoma Jiji ilirejea kwa nguvu na kufanikiwa kusawazisha mabao dakika ya 88 kupitia Dickson Ambundo aliyepenya safu ya ulinzi ya Yanga kabla ya kutikisa nyavu.
Dakika ya 90, makosa ya safu ya ulinzi ya Yanga yalitoa nafasi kwa Waziri Junior kufunga bao la ushindi na kuhitimisha ushindi mkubwa kwa Dodoma Jiji.
Licha ya kupoteza mchezo huo, Yanga inaendelea kuongoza msimamo wa ligi ikiwa na pointi 54 baada ya kucheza mechi 23, huku watani wao Simba SC wakifuatia kwa pointi 49 katika idadi sawa ya mechi.

Iwapo Simba SC itaibuka na ushindi dhidi ya Mashujaa FC katika mchezo wa Mei 14, 2026, tofauti ya pointi kati yao na Yanga itapungua hadi pointi mbili pekee, hali inayozidi kupamba moto mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
