Moja ya mechi ya mashindano ya mbuzi ambayo yalifanyika jijini Dar es salaam na kuwa kivutio kwa watazamaji wengi
Mashindano hayo yaliambatana na burudani mbalimbali katika viwanja vya Oysterbay.
Wadau mbalimbali wakifurahia ushindi kwa kupiga picha na mbuzi washindi.
………………….. 

 Katika mwendelezo wa dhamira ya kuboresha sekta ya elimu nchini, kampuni ya Barrick nchini, imeunga mkono klabu ya Rotary kudhamini mashindano ya mbuzi ambayo yalifanyika jijini Dar es Salaam.

Mashindano hayo yanayofanyika kila mwaka kwa ajili ya kupata fedha za kuunga mkono jitihada za Serikali kupambana na changamoto mbalimbali katika jamii, mwaka huu yamelenga kusaidia kuboresha mazingira ya elimu na kuwasomesha watoto wenye mazingira magumu ambao wanakosa  fursa za kupata elimu.

Barrick Imekuwa mstari wa mbele kuunga mkono jitihada za Serikali kuboresha sekta ya elimu ambapo kupitia fedha za uwajibikaji kwa jamii zinazotolewa na migodi yake ya North Mara na Bulyanhulu zimefanikisha miradi mbalimbali ya ujenzi wa  miundombinu ya shule na vyuo katika maeneo yanayozunguka migodi hiyo,

Kuanzia mwaka jana kwa kushirikiana na Serikali imeanza kutekeleza  mradi wa kusongesha mustakabali wa elimu nchini unaojulikana kama ‘Barrick-Twiga Future Forward Education Program’ ambao katika awamu yake ya kwanza umefanikisha  ujenzi wa miundombinu ya madarasa na mabweni ya kisasa na vyoo katika shule za sekondari za Serikali katika mikoa mbalimbali nchini.