Na John Bukuku, Dodoma

Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema uhifadhi wa mazingira ni jukumu la kila mwananchi, kwa kuwa athari za uharibifu wa mazingira huathiri moja kwa moja maisha ya binadamu pamoja na maendeleo ya taifa.

Dkt. Semesi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wanafunzi katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika jijini Dodoma.

Amesema NEMC inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali inayolenga kubadili mtazamo wa wananchi kuhusu taka, kwa kuzigeuza kuwa fursa za kiuchumi kupitia ukusanyaji, uchakataji na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zinazotokana na taka.

Kwa mujibu wa Dkt. Semesi, hatua hiyo inalenga kusaidia kulinda mazingira huku ikiongeza kipato kwa wananchi kupitia shughuli za urejelezaji na uchumi wa mzunguko.

Aidha, amesema NEMC imejipanga kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhifadhi mazingira ili yaendelee kutoa huduma muhimu za kiikolojia, fursa za kiuchumi na kuchangia maendeleo endelevu ya nchi.

Ameongeza kuwa maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yamekuwa jukwaa muhimu la kuelimisha umma kuhusu masuala ya mazingira pamoja na kutoa ushauri wa kitaalamu unaolenga kuboresha huduma za usimamizi na uhifadhi wa mazingira nchini.

Dkt. Semesi amewahimiza wanafunzi na wananchi kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika shughuli za utunzaji wa mazingira, ikiwemo upandaji miti, usimamizi bora wa taka na matumizi endelevu ya rasilimali za asili ili kuhakikisha mazingira salama kwa kizazi cha sasa na kijacho.