Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya makaazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Rahma Kassim Ali na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi (Mb.), wametembelea Ubalozi wa Tanzania nchini Namibia na kufanya kikao kazi na watumishi wa Ubalozi.
Awali Balozi wa Tanzania Nchini Namibia, Mhe. Caesar Waitara aliwatembeza viongozi hao kukagua Ofisi za Ubalozi na kuwaeleza mipango waliyonayo katika kuboresha utendaji kazi wa Ubalozi.
Waziri Rahma amaushukuru Ubalozi kwa utekelezaji mzuri wa Diplomasia ya Uchumi na maandalizi wanayofanya kwa ajili ya kumpokea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Hassan Suluh ambaye anatarajia kufanya ziara ya kikazi ya siku moja nchini Namibia pamoja na kuwa Mgeni Rasmi wa Sherehe za Uapisho wa Rais Mteule wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Nandi-Ndaitwah.
Aidha, Rais Samia anatarajiwa kuhutubia kwenye sherehe hizo za uapisho zitakazofanyika pamoja na maadhimisho ya Miaka 35 ya Uhuru wa Jamhuri ya Namibia.
Tanzania na Namibia wanamahusiano mazuri yaliyoasisiwa na Hayati Julius Nyerere na Hayati Sam Nujoma kipindi cha harakati za ukombozi wa nchi za Kusini mwa bara la Afrika.