Baadhi ya Washiriki wa Michezo ya Wakuu wa Majeshi  ya Polisi kusini mwa Afrika (SARPCCO) yaliyayofanyika katika jiji la Windhoek  nchini Namibia mwaka 2013 wakiwa katika picha ya pamoja.Picha na Polisi

…………………………..

Na A/INSP Frank Lukwaro

Timu za Jeshi la Polisi Tanzania zitakazoshiriki michezo ya 11 ya Umoja wa Wakuu wa Majeshi ya Polisi kwa nchi za kusini mwa Afrika (SARPCCO),  kuanzia Septemba 3, 2022 jijini Dar es Salaam  zinaendelea kujifua vyema katika  kambi yao inayoendelea katika Shule ya PolisiTanzania- Moshi.

Mkuu wa kitengo cha  michezo cha Jeshi la Polisi, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Jonas Mahanga alizitaja timu zilizopo kambini kuwa ni  pamoja na Timu ya Mpira wa miguu, pete,Wavu, riadha, chess na vishale ambapo hivi sasa zinajifua kuhakikisha kuwa zinakuwa vizuri pindi michuano hiyo itakapoanza kutimua vumbi ambapo Tanzania ndio mwenyeji.

Amesema timu hizo zinaendelea kucheza michezo ya kirafiki ili kujipima nguvu na kuhakikisha wanafanya vizuri kwa kuwa michezo ya mwaka huu itakuwa na ushindani mkubwa kutokana na nchi zilizothibitisha kushiriki kujipanga vizuri.

ACP Mahanga alizitaja nchi zilizothibitisha kushiriki kuwa ni Afrika Kusini, Angola, DRC Kongo, Eswatini, Lesotho, Malawi, Msumbiji, Namibia, Shelisheli, Zambia, Zimbambwe na mwenyeji Tanzania ambapo alivitaja viwanja vitakavyotuika kuwa ni pamoja na  Benjamini Mkapa, Uhuru, JK Park, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Gwambina.

Kwa upande wake kocha  wa timu ya mpira wa miguu Sajenti Yusuph Ramadhan amesema wachezaji wake wamekuwa wakionesha kiwango kizuri katika mazoezi kwa kuwa wamekaa kwa muda mrefu na wana uzoefu ambao utawafanya wawezekufanya vizuri katika michezo hiyo.

Naye Mwalimu wa timu ya mpira wa pete Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Edson Chitanda amesema mazoezi yake yamelenga kuwafanya wachezaji wake kuwa kasi ili kuweza kuwakabili timu shindani na zenye historia ya kufanya vizuri katika michezo hiyo.