Na Mwandishi wetu,
Wakulima wa zao la Korosho wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia pembejeo za kilimo licha ya uwepo wa changamoto mbalimbali.
Wakulima hao ambao ni Wakulima wa Korosho wa mkoa wa Mtwara wameendelea kupokea pembejeo za kilimo ikiwemo dawa za maji na dawa ya unga ama Sulphur ambapo hawakusita kupaza sauti zao za pongezi.
“Sisi Wakulima tunatambua jitihada za Rais Samia kutupa pembejeo ambapo hatujaamini kama tungepata kutokana na namna Wakubwa huko Ulaya wanavyopigana vita na hivyo kupelekea uzalishaji kupungua na kupata huku dawa ni Maajabu ambayo Rais Samia ameonyesha namna anavyotupambania sisi Wakulima.” alisema Mwananchi ambaye pia ni Mkulima Ndugu Rashid Hamid maarufu kwa jina la Mkapa mkazi wa Nansinji.
Hayo yamejili wakati wa ziara aliyofanya Ndugu Emmanuel Shilatu ambaye ni Afisa Tarafa kujiridhisha juu ya mwenendo wa ugawaji wa pembejeo ambapo zoezi limeendelea vyema.
“Kwa niaba ya Wananchi ningependa kuungana nao kumpongeza Mhe. Rais Samia kwa namna anavyowajali Wakulima kwa kuwapatia pembejeo za kilimo. Anayafanya hayo sanjali na kuwapatia Wataalamu wa kilimo, kuwapatia mbegu na kuwasimamia Wakulima kupata masoko ya mazao Yao kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani. Hauwezi kuongelea mafanikio ya Kilimo na Wakulima nchini pasipo kumtaja Rais Samia.” Alisema Shilatu
Halikadhalika Mwenyekiti Kijiji Cha Kivukoni Ndugu Jackson Joseph Milanzi alishukuru kwa pembejeo na kuhaidi kutekeleza maelekezo ya Afisa Tarafa ya kuendelea kusimamia ugawaji wa pembejeo hizo kwa uwazi, haki na usawa kama zoezi linavyoendelea.
Wakulima wa Korosho nchini wameanza kupokea pembejeo za kilimo mapema sana kwa msimu huu tofauti na hapo awali na hivyo wanatarajia kuwa na msimu mzuri wa Korosho kwa mwaka huu na hivyo kupata tija ya uzalishaji.

