NA MWANAMICHEZO WETU,  NOEL RUKANUGA 

Simba SC  imeendeleza ubabe wake katika Ligi Kuu ya NBC baada ya leo, Jumatano, Juni 17, 2026, kuichapa Mbeya City bao 1-0 katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Ushindi huo umeifanya Simba kupanda kileleni mwa msimamo wa ligi kwa kufikisha pointi 64, na hivyo kuendelea kuweka hai matumaini yake ya kutwaa ubingwa wa msimu huu.

Kwa kufunga bao hilo la ushindi, Mpanzu ameendelea kuwa katika kiwango bora baada ya kufumania nyavu za wapinzani katika mechi tatu mfululizo.

Kabla ya mchezo wa leo, alikuwa tayari amefunga dhidi ya Dodoma Jiji na Pamba Jiji. Huu ni ushindi wa saba mfululizo kwa Simba katika Ligi Kuu tangu ilipotoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya Yanga mnamo Mei 3 mwaka huu.

Baada ya bao hilo, timu zote mbili zilishambuliana kwa zamu, lakini ubao wa matokeo haukubadilika hadi filimbi ya mwisho ilipopulizwa na mwamuzi Ahmada Simba kutoka Kagera.

Kwa upande mwingine, matokeo hayo yameizidishia Mbeya City presha katika vita vya kujinusuru kushuka daraja. Timu hiyo imebakiza mechi tatu muhimu dhidi ya Dodoma Jiji, Pamba Jiji na TRA United ambazo zitakuwa za maamuzi katika hatma yake.

Baada ya mchezo wa leo, Simba itageukia mechi ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB dhidi ya Coastal Union itakayochezwa katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha, Jumamosi, Juni 20.

Kwa upande wa Mbeya City, itashuka tena dimbani Juni 24 katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Pamba Jiji utakaopigwa katika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.