Mkurugenzi wa House of Canvas Ltd, Evans Ogiloh akizungumza na waandishi wa habari kwenye maonesho hayo.
………..
Na Happy Lazaro, Arusha .
Maonesho ya Karibu-Kilifair 2026 yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wadau wa sekta ya utalii na biashara, huku yakitoa nafasi kwa kampuni mbalimbali kutangaza bidhaa na huduma zao kwa masoko ya ndani na kimataifa.
Mkurugenzi wa House of Canvas Ltd, Evans Ogiloh, amesema kampuni hiyo imeshiriki maonesho hayo ikiwa na lengo la kuonesha ubora wa bidhaa zake zinazotumika katika shughuli za utalii na kambi mbalimbali, huku akiwakaribisha wadau kutembelea banda lao na kujionea bidhaa hizo.
Akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho hayo yanayoendelea jijini Arusha, Ogiloh amesema mwaka huu wamekuja na bidhaa mpya na za kisasa zaidi zikiwemo mahema ya kitalii, mahema ya milimani na vifaa vingine vya kambi vilivyotengenezwa kwa viwango vya juu vya ubora na vinavyodumu kwa muda mrefu.
Amesema maandalizi ya Karibu-Kilifair 2026 yameonesha mafanikio makubwa katika kukuza sekta ya utalii na biashara, akibainisha kuwa waandaaji wameweka mazingira bora yaliyowezesha washiriki wengi zaidi kufikia wateja na washirika wa biashara.
“Tumefurahishwa sana na namna maonesho yalivyoandaliwa mwaka huu. Yamekuwa makubwa zaidi na yameibua fursa nyingi za kibiashara kwa washiriki. Hii inaonesha namna sekta ya utalii inavyoendelea kukua na kuvutia wadau wengi zaidi,” amesema Ogiloh.
Ameeleza kuwa House of Canvas Ltd imeendelea kujikita katika utengenezaji wa mahema na vifaa vya kambi vinavyokidhi mahitaji ya kampuni za utalii, wapandaji milima na taasisi mbalimbali, huku ikichangia kukuza matumizi ya bidhaa zinazozalishwa nchini.
Aidha, amesema maonesho hayo yamekuwa nyenzo muhimu ya kuitangaza Arusha kama kitovu cha utalii na biashara za utalii Afrika Mashariki, huku yakifungua milango ya ushirikiano mpya kati ya wafanyabiashara wa ndani na wageni kutoka mataifa mbalimbali.
Amesema moja ya vipaumbele vya kampuni hiyo ni kuendelea kubuni na kuzalisha bidhaa zinazokidhi mahitaji ya soko la kisasa la utalii, huku wakizingatia viwango vya ubora, usalama na uimara unaohitajika katika mazingira mbalimbali ya shughuli za utalii na kambi.
Pia ameeleza kuwa ushiriki wao katika maonesho ya Karibu-Kilifair umeendelea kuwa chachu ya ukuaji wa biashara kwa kuwapatia fursa ya kukutana na wateja wapya, wawekezaji pamoja na wadau wa sekta ya utalii kutoka ndani na nje ya Tanzania, jambo ambalo limechangia kuimarisha mtandao wa biashara na kuongeza uhitaji wa bidhaa zao katika masoko mbalimbali.

