Na Mwandishi Wetu, TANGA
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi ,Dkt Batilda Burian, amewaasa wananchi wa mkoa huo kuendelea kudumisha amani na utulivu wakati wa Sikukuu ya Eid Al-Adha
Aliyasema hayo leo mara baada ya kumalizika swala ya Eid Al-Adha iliyofanyika katika msikiti wa Ijumaa Jijini Tang ambapo alisema ni kill muhimu kwa Waislamu na wananchi kwa ujumla kuendelea kuonesha mshikamano kwa kuwasaidia watu wenye uhitaji, wakiwemo majirani, watoto wanaoishi katika vituo vya yatima pamoja na wajane, ili kila mmoja aweze kusherehekea sikukuu hiyo kwa furaha.
Aidha, aliwataka wananchi wa Mkoa wa Tanga kuendelea kudumisha amani na kuhakikisha watoto wanakuwa salama kipindi cha sikukuu, hasa wanapokwenda kutembea au kuogelea ufukweni.
Alisisitiza kuwa watoto wanapaswa kusimamiwa na watu wazima ili kuepusha ajali zinazoweza kujitokeza, ikiwemo ajali za bodaboda, magari pamoja na maji kwa watoto wasiokuwa na ujuzi wa kuogelea.
“Ni muhimu kuhakikisha sikukuu yetu inaisha salama huku tukiendelea kumuomba Mwenyezi Mungu atujalie amani na kutuongoza katika mema,” alisema.
Pia alimpongeza Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, pamoja na viongozi wengine wa serikali, akiomba Mwenyezi Mungu aendelee kuwapa afya njema, hekima na umri mrefu ili waendelee kuiongoza nchi kwa amani, utulivu na maendeleo.
Kwa upande wake, Shehe wa Mkoa wa Tanga, Jumaa Luwuchu, amesema dini inasisitiza amani na upendo, huku akibainisha kuwa hakuna sehemu yoyote inayoruhusu uvunjifu wa amani.
Amesema waumini wanapaswa kuendelea kufanya matendo mema, kushikamana na kuwasaidia wasiojiweza kwani hayo ni miongoni mwa mambo muhimu katika ibada na mafunzo ya dini ya Kiislamu.
