Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) akisalimiana na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.

Na. Peter Haule, WF, Nairobi, Kenya

Tanzania na Marekani zimeeleza dhamira ya kuendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali za maendeleo, ikiwemo afya, kilimo, nishati, madini, miundombinu, elimu na utalii.

Dhamira hiyo imeelezwa wakati Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokutana na kufanya mazungumzo na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Luswetula amezialika kampuni na wawekezaji kutoka Marekani kutumia fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana Tanzania, akitaja maeneo ya kilimo, nishati, madini, miundombinu, afya, elimu na utalii.

Aidha, Mhe. Luswetula ameishukuru Serikali ya Marekani kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania pamoja na mchango wake katika maeneo mbalimbali ya maendeleo tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mwaka 1968.

Amesema ushirikiano huo umekuwa na mchango katika juhudi za Tanzania za kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi na kupunguza umaskini.

Kwa upande wake, Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, amesema Marekani itaendelea kushirikiana na Tanzania katika maeneo mbalimbali ya maendeleo, pamoja na kuimarisha na kukuza ushirikiano uliopo baina ya nchi hizo.

Mazungumzo hayo yameangazia pia umuhimu wa kuendelea kujenga ushirikiano wa kiuchumi na uwekezaji kati ya Tanzania na Marekani kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizo mbili.