Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewasili leo, tarehe 30 Agosti 2026, jijini Belgrade, Jamhuri ya Serbia, kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Maalum wa Ngazi ya Juu wa Kumbukumbu ya Miaka 65 tangu kufanyika kwa Mkutano wa Kwanza wa Wakuu wa Nchi wa Harakati za Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM).
Rais Dkt. Mwinyi amewasili akiwa ameambatana na ujumbe wake, akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, pamoja na viongozi wengine wa Serikali.
Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Nikola Tesla, Rais Dkt. Mwinyi amepokelewa na Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Uchumi wa Jamhuri ya Serbia, Mhe. Adrijana Mesarović, pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Italia ambaye pia anaiwakilisha Tanzania katika Jamhuri ya Serbia, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.

