Na Mwandishi Wetu, Dodoma. 

ZAIDI ya washiriki 1,000 kutoka Bunge, wizara 14 na taasisi 10 wanatarajiwa kushiriki NMB Bunge Bonanza 2026 litakalofanyika Jumamosi jijini Dodoma, baada ya NMB Bank Plc kukabidhi udhamini wake wathamani ya Sh milioni 210 ikiwemo vifaa vya michezo kwa ajili ya mashindano hayo.

Mwenyekiti wa Bunge Bonanza na Mbunge wa Makete, Festo Sanga, amesema mwaka huu Spika wa Bunge, Mussa Azzan Zungu, amealika wizara 14 na taasisi nyingine 10. Idadi ya washiriki inatarajiwa kuwa kubwa kuliko miaka iliyopita, huku akiongezea bonanza hilo litafanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari John Merlini, jijini Dodoma, Jumamosi, Agosti 29, 2026.

Mshauri Mwandamizi wa Kitengo cha Biashara za Serikali Benki ya NMB, Vicky Bishubo, amesema benki inaunga mkono michezo kwa sababu ya mchango wake katika afya, mshikamano na tija kazini. Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na mipira, makombe, track suti za michezo, fulana na medali.

Spika Zungu anatarajiwa kuwa mgeni rasmi. Kabla ya bonanza kuanza, wabunge watafanya matembezi yatakayoanzia Chuo cha Mipango saa 12:00 asubuhi. 

Ingawa ushindani mkali unatarajiwa kutoka kwa timu za Bunge, wizara, taasisi na NMB, Sanga alisema lengo kuu ni kuwavuta watumishi kwenye mazoezi, kujenga mshikamano na kuongeza uelewa kuhusu kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza