Na Waandishi Wetu
Vita mpya imeanza katika ukanda wa Afrika Mashariki. Sio vita vya bunduki wala migogoro ya mipaka. Ni vita vya miundombinu, viwanja vya ndege, barabara na masoko baina ya nchi za Tanzania na Kenya katika kuvutia watalii. Kwa upande wake Serikali ya Kenya ipo katika ujenzi wa uwanja wa ndege wa KSh Bilioni 1.4 unaojengwa pembezoni mwa Maasai Mara.
Wakati huo huo, Serikali ya Tanzania bado ikijipanga kuanza mchakato wa ujenzi wa uwanja wake wa kimataifa wa Serengeti. Ushindi wa vita hii utaamua wapi fedha za watalii zitakapotiririka kwa wingi, hususani katika muongo ujao. Na kwa kuwa Serengeti na Mara zinashiriki mfumo mmoja wa ikolojia, mshindi atapata zaidi ya watalii. Atapata hadithi, ajira na uchumi.
Kwa wiki moja timu ya waandishi ilifanya uchunguzi wa kina nchini Kenya. Tulitoka Nairobi hadi Narok town, kisha hadi Talek, na tukafika ndani ya kilomita 30 za milango ya Sekenani na Oloololo. Kila mtu tuliemzungumza, kuanzia maafisa wa kaunti, wahandisi, madereva wa safari, hadi wasimamizi wa kambi, alikuwa na ujumbe mmoja. Kenya haijengi uwanja tu. Inajenga “mlango wa mbele” wa Uhamiaji Mkubwa wa Wanyamapori. Kwa lugha nyingine ujenzi huo umelenga kuwavutia watalii washukie moja kwa moja nchini Kenya na kuanzia safari yao huko.
Uwanja wa ndege wa Narok kwa mujibu wa nyaraka rasmi za Mamlaka ya Viwanja vya Ndege vya Kenya na Serikali ya Kaunti ya Narok, utakuwa na barabara ya ndege ya kilomita 1.5 inayoweza kutua ndege za kati na za charter. Pia utakuwa na kituo cha kisasa cha abiria chenye ofisi za uhamiaji na forodha, ghala la mizigo na vifaa vya chaini ya baridi, maeneo ya maegesho ya ndege, njia za kutaxi, pamoja na mfumo kamili wa usalama wa anga. Ujenzi ulianza katikati ya mwaka 2025 na tayari uko asilimia 35. 
Wasimamizi wa eneo hilo walisema awamu ya kwanza inatarajiwa kukamilika Desemba 2027 kwa bajeti ya KSh Bilioni 1.4 ambayo inaghawiwa na serikali ya kitaifa na ya kaunti.
Lakini pamoja na ujenzi wa uwanja wa ndege, Kenya ipo mbele kidogo katika maeneo mengine muhimu. Kwanza ni barabara. Barabara ya Narok hadi Sekenani inapanuliwa na kufanyiwa lami. Kwa sasa inachukua masaa 3 kufika langoni. Serikali ya kaunti inasema ukikamilika utachukua dakika 45 tu. Pili ni malazi. Afisa wa mipango wa kaunti alituambia kuwa katika miezi 18 iliyopita wameidhinisha ujenzi wa kambi 12 mpya za kifahari katika maeneo ya Talek na Ololaimutia. Wawekezaji binafsi wameona ishara na wameanza kuweka pesa zao.
Tatu ni masoko. Bodi ya Utalii ya Kenya tayari imeanza kazi. Bodi hiyo ilisema wameshaanza kuwasilisha kwa waendeshaji wa utalii ‘Tour Operators’ wa London, Frankfurt na New York kwa kutumia kauli mbiu ya “Fly Direct to the Mara” kwa ajili ya msimu wa 2028. Vitabu vyao vya matangazo tayari vinaonyesha picha ya uwanja wa Narok kama umekamilika. Nne ni motisha za kifedha. Serikali ya kaunti imeidhinisha punguzo la kodi za kutua kwa mashirika yote ya ndege yatakayoruka moja kwa moja Narok. Lengo ni wazi: kuvuta ndege na watalii waondoke Nairobi.
Afisa mkuu wa Idara ya Utalii ya Kaunti ya Narok alifupisha mkakati wao kwa ufasaha. “Kwa miaka mingi tulikuwa tunawaangalia watalii wakifika Nairobi, kulala hoteli moja mjini, kisha kusafiri masaa 6 kwa barabara hadi kwetu. Kwa nini mtalii anayelipa dola 800 kwa usiku atumie nusu siku yake akiwa safarini? Kwa uwanja huu, atatua dakika 20 kutoka langoni. Muda huo na pesa hizo zote zitabaki Kenya.”
Hii ndipo Serengeti inapoingia kwenye kivumbi kikali na Maasai Mara. Serengeti na Maasai Mara ni mfumo mmoja wa ikolojia wenye ukubwa wa kilomita za mraba 25,000. Wanyama, hasa wimbi la wanyamapori, wanavuka Mto Mara bila kujali mipaka wala pasipoti. Lakini watalii hawana bahati hiyo. Watalii wanafuata ndege, wanafuata barabara, na wanafuata urahisi. Na hapo ndipo hatari kubwa ilipo kwa Tanzania.
Takwimu zinaonyesha ukubwa wa pato linalohusika. Kwa mujibu wa Bodi ya Utalii Tanzania, mwaka 2023 Serengeti ilipokea watalii zaidi ya 450,000 na kuzalisha zaidi ya TSh Trilioni 1.2. Kwa upande wa Kenya, takwimu rasmi zinaonyesha Maasai Mara ilipokea watalii takriban 320,000 katika mwaka huo huo. Tofauti iko, lakini soko ni moja.
Kenya sasa inakadiria kuongeza idadi ya watalii waenda Mara kwa asilimia 40 ndani ya miaka mitatu ijayo. Pia inakadiria kuelekeza asilimia 25 hadi 30 ya trafiki ya watalii wanaovuka kutoka Kenya kwenda Tanzania. Kama makadirio hayo yakatimia, wachambuzi wanasema Tanzania inatarajiwa kupoteza kati ya TSh Bilioni 300 hadi 360 kila mwaka. Pesa hiyo ni sawa na bajeti ya miradi kadhaa ya maendeleo mikoani.
KENYA INAVYOICHANGAMKIA SERENGETI
Ukweli mchungu ni kwamba Kenya sasa inafanya kila juhudi kuhakikisha inafaidika na utalii wa Serengeti bila mtalii hata mmoja kukanyaga Tanzania. Kupitia uwanja wa Narok, barabara mpya, na matangazo makali, Kenya inajiuza kama “lango rasmi la Uhamiaji Mkubwa”. Hii ni licha ya ukweli kwamba asilimia 80 ya uhamiaji huo unaanzia na kumalizikia ndani ya mipaka ya Tanzania. Mkakati wao ni wazi. Mtalii akishuka Narok, atafanya safari zake zote ndani ya Kenya. Pesa zake zote zitabaki Kenya. Hii ndiyo vita tunayopaswa kuielewa.
Waendeshaji wa utalii Nairobi walizungumza nasi bila kificho. “Wateja wetu hawajali mipaka,” alisema James Okoth, Mkurugenzi Mtendaji wa Johnson Elite Safaris. “Wanajali kuona simba, kifaru na twiga. Wanajali kufika hoteli kabla ya jua kuchwa. Kama Kenya inafanya iwe rahisi zaidi, sisi tutauza Kenya. Ni biashara tu.”
Asha Juma wa East Africa Tours aliongeza kwa ukweli zaidi. “Hesabu ni rahisi sana. Ndege ya moja kwa moja hadi Narok na kulala usiku 2 Mara ni nafuu na rahisi zaidi kuliko kuruka hadi Arusha na kisha kusafiri masaa 6 kwa gari kwenda Serengeti. Tutaiacha Tanzania kwenye nusu ya vifurushi vyetu ifikapo 2028 kama hakutakuwa na mabadiliko.”
RAIS SAMIA AKIONGOZA NA WIZARA KUWEKA MSIMAMO
Jijini Dodoma, Serikali ya Tanzania chini ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ilipongezwa na wadau wote wa sekta kwa uamuzi wake wa kishujaa wa kutoa amri kwa Wizara ya Uchukuzi kuharakisha mipango ya ujenzi wa Uwanja wa Kimataifa wa Serengeti katika Mkoa wa Mara. Katika hotuba ya bajeti ya Wizara ya Uchukuzi ya 2025/2026 tayari imetengwa fedha kwa ajili ya kufanya utafiti wa kina, tathmini ya athari za mazingira na kuandaa mpango mkuu. Wizara pia imeweka msimamo wazi kwamba uwanja huu lazima ujengwe na lazima ujengwe kwa wakati.
Uwanja umepangwa kuwa na barabara ya ndege ya kilomita 2.0 karibu na eneo la Seronera. Lengo ni ili uweze kutua ndege kubwa za abiria na ndege za charter za moja kwa moja kutoka Ulaya na Marekani.
“Rais Samia lazima apongezwe kwa uongozi huu. Hili ni suala la kulinda rasilimali yetu na uchumi wetu. Hatuna budi kuhakikisha mtalii anapofika Afrika Mashariki, anaanzia Tanzania. Serengeti ni yetu na lazima Watanzania wafaidike kwanza,” alisema Juma Hamis, mdau wa sekta ya utalii.
Pongezi pia zinaelekezwa kwa Wizara ya Uchukuzi kwa kuonyesha msimamo na kasi. Uamuzi wa kutenga fedha na kuanzisha michakato mapema unaonyesha Serikali imeelewa ukubwa wa tishio hili na fursa iliyopo.
KIKWAZO: WATANZANIA WACHACHE WANAOPINGA
Licha ya umuhimu huu wa kitaifa, uchunguzi wetu umebaini kuwa bado wapo Watanzania wachache wanaopinga mradi huu kwa maslahi yao binafsi. Wengine wanadai kuhusu mazingira bila kutoa mbadala, huku wengine wakidaiwa kutumiwa kutoka nje ya nchi ili kuudhofisha mradi huu muhimu.
Wadau wa sekta wanasema ni wakati wa kuacha siasa na maslahi binafsi na kuangalia maslahi ya taifa. “Tunaambiwa tuhifadhi, lakini tunapofungwa mikono ya kujenga miundombinu, Kenya inakuja na kuchukua watalii wetu. Hapo ndipo uhifadhi unapokufa kwa kukosa fedha,” alisema mmoja wa viongozi wa TATO.
Lakini wadau wengine kutoka sekta ya utalii nchini wanasema kasi ya maandalizi ya ujenzi wa uwanja wa ndege Serengeti ndiyo kila kitu sasa. “Kenya ipo mbele zaidi yetu kwa takriban miaka miwili kwenye mkakati huu wa kuvutia watalii,” alisema Dkt. Neema Emmanuel, mchumi na mtaalamu wa utalii kutoka Dar es Salaam. “Kama Tanzania itasubiri hadi 2028 kuanza ujenzi, basi tutapoteza soko kwa muongo mzima. Serikali lazima iharakishe vibali, ipate fedha, na ianze ujenzi robo ya kwanza ya 2027. Huu sio wakati wa kufuata utaratibu mrefu wa kiserikali. Huu ni ushindani wa kiuchumi.”
William Munisi, mwanachama wa Chama cha Waendeshaji Utalii Tanzania TATO, alizungumza kwa uchungu zaidi. “Tunaomba Serikali: tafadhali harakisha. Kila mwezi wa kuchelewa ni pesa inayopotea na kwenda moja kwa moja Kenya. Tunataka uwanja huo wa Serengeti ufanye kazi ifikapo 2029. Tukifanya hivyo hatutakuwa tunafuatilia tu. Tutawapita kwa sababu Uhamiaji wa wanyama unaanzia Serengeti. Watalii wanataka kuanzia pale tukio linapotokea, sio kufika baadae.”
Hans Mbwaga, Mkurugenzi Mtendaji wa Hans Trails Ltd aliyeko Arusha, alisema kitu ambacho kinawauma waendeshaji wengi. “Kwa sasa ninauza Kenya kwa sababu ni rahisi kwa mteja. Nipe uwanja wa kimataifa Serengeti na nakuahidi nitawaleta wateja 1000 zaidi mwaka ujao. Mahitaji yapo. Watalii wanataka kuja. Serikali inatakiwa tu kutoa miundombinu.”
Faida za kuwa na uwanja wa kimataifa upande wa Tanzania ni nyingi na ni za papo hapo na za muda mrefu. Ya kwanza ni upatikanaji. Kwa sasa inachukua masaa 6 kutoka Arusha hadi Seronera kwa barabara. Ukiwa na uwanja Serengeti, safari hiyo itakuwa ndege ya dakika 50. Tutakuwa tumelingana na Kenya lango kwa lango.
Ya pili ni mapato. Ambapo uboreshaji wa upatikanaji unaweza kuongeza makusanyo ya ada za hifadhi kwa hadi asilimia 40 ndani ya miaka mitano. Ndege zaidi maana yake vitanda zaidi kujazwa, na ada zaidi kulipwa na serikali kupata mapato.
Ya tatu ni ajira. Ujenzi peke yake utatoa ajira kwa watu zaidi ya 2,000. Ukiwa umekamilika na unafanya kazi, kuna matarajio ya ajira 5,000 za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja katika Mkoa wa Mara. Hii ni kimbilio kwa vijana wetu.
Ya nne ni maendeleo ya kikanda. Uwanja huu sio wa watalii tu. Utafungua mji wa Musoma na Ukanda wote wa Ziwa kwa ajili ya usafirishaji wa mizigo, biashara, na hata safari za matibabu. Utatuunganisha na dunia.
Ya tano na muhimu zaidi ni udhibiti wa hadithi. “Uhamiaji Mkubwa unaanzia Ndutu, Tanzania,” alisema mwongozaji wa watalii mzoefu Emmanuel John. “Lakini kwa miaka mingi Kenya imekuwa ikiuza hadithi hiyo vizuri zaidi kwa sababu ni rahisi kufika. Uwanja Serengeti utaturudishia hadithi yetu. Sisi ndio nyumbani kwa Uhamiaji. Lazima tuimiliki.
Miezi 24 ijayo ndiyo itakayoamua nani atashinda vita hii. Wakati Kenya inamwaga saruji Katika ujenzi wa uwanja huo wa ndege wa Narok na kuanza kutangaza msimu wa 2028, Tanzania bado iko katika awamu ya usanifu na uidhinishaji wa mradi wa Serengeti. “Mbio zimeanza,” alisema mhandisi wa KAA tulipokuwa tunatoka eneo la ujenzi Narok. “Itashinda nchi itakayemaliza kwanza na kuitangaza zaidi.
Uchunguzi wetu umethibitisha kuwa hii sio tena mazungumzo ya wanyamapori peke yake. Ni mazungumzo ya miundombinu, sera za anga, masoko, na uzoefu wa mgeni.
Uamuzi wa Rais Samia wa kusonga mbele na Uwanja wa Serengeti kwa hiyo sio tu jibu la kiulinzi. Ni tamko la kimkakati. Kama alivyosema Ally Nasri, Mchumi kutoka Dodoma, “Hii ni kulinda sehemu yetu. Serengeti ni ya Tanzania, na Watanzania lazima wafaidike kwanza.”
Lakini ujumbe kutoka kwa sekta binafsi ni wazi na ni wa dharura: Tenda sasa. “Serikali lazima iufanye mradi wa ujenzi wa uwanja wa ndege Serengeti kama mradi wa dharura wa kitaifa,” alisisitiza Emmanuel Samson, mwongozaji wa watalii mzoefu. “Punguza utaratibu mrefu na milolongo. Leta wawekezaji wa PPP. Lengo liwe kufungua kabla ya Kenya. Ndiyo njia pekee ya kuwapita.”
Alimalizia kwa kusema, “Tuna bidhaa bora zaidi duniani. Hakuna mahali pengine duniani penye Uhamiaji kama wetu. Tunachohitaji sasa ni uwanja bora zaidi wa kuuleta ulimwengu kwetu. Mheshimiwa Rais, tafadhali harakisha. Acha Tanzania iongoze, sio kufuata.”
Kuhakikisha kuwa watalii wanaweza kutua moja kwa moja ndani ya mipaka ya Tanzania ndiyo ufunguo wa kulinda mapato ya nchi, kulinda ajira za vijana, na kulinda mustakabali wa uhifadhi ambao sekta ya utalii inategemea.
