Mshambuliaji chipukizi wa Hispania, Lamine Yamal, alikuwa kivutio kikubwa wakati wa gwaride la mabasi ya wazi jijini Madrid baada ya taifa hilo kutwaa Kombe la Dunia 2026.

Hispania ilirejea nyumbani ikiwa bingwa wa dunia kufuatia ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Argentina katika fainali iliyochezwa Jumapili, na kuongeza nyota ya pili kwenye jezi yao.

Mashujaa hao walipokelewa kwa shamrashamra kubwa na takribani mashabiki milioni mbili waliovalia rangi za taifa, huku wakipeperusha bendera na kubeba mabango yaliyotawala mitaa ya Madrid.

Katika hali ya furaha, Yamal, mwenye umri wa miaka 19, alionyesha kipaji chake cha kucheza muziki akiwa juu ya basi la wazi.
Nyota huyo wa Barcelona alishirikiana na winga wa Athletic Bilbao, Nico Williams, ambapo wawili hao walionyesha miondoko ya kuvutia iliyowasisimua maelfu ya mashabiki waliojitokeza kusherehekea ushindi huo.

Wachezaji wengine walionekana wakiwa wamevua fulana, wakijifunika bendera ya Hispania huku wakifurahia shamrashamra za ubingwa.

Mshambuliaji mkongwe Borja Iglesias naye alichukua jukumu la kuwa DJ wa kikosi, akisimamia muziki uliowafanya wachezaji na mashabiki kuendelea kushangilia katika sherehe hizo.