Na. Antonia Mbwambo-Dodoma

Tarehe 24 Juni, 2026

Timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI kwa kushirikiana na Watumishi Housing Investment (WHI) imefanya ziara ya ukaguzi wa miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi awamu ya pili katika Wilaya ya Dodoma, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa kuzingatia ubora, thamani ya fedha na ratiba iliyopangwa.Ziara hiyo iliongozwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Bw. Patrick Allute, ambaye amesema Serikali inaendelea kuimarisha mazingira ya kazi na makazi ya watumishi wa umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bw. Allute alisisitiza umuhimu wa usimamizi madhubuti wa miradi, matumizi sahihi ya rasilimali za umma na ukamilishaji wa kazi kwa wakati huku viwango vya ubora vikizingatiwa. Pia alielekeza changamoto zilizobainika kushughulikiwa kwa haraka ili kuhakikisha malengo ya miradi yanafikiwa kama ilivyopangwa.Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unatoa matokeo yanayokusudiwa kwa manufaa ya watumishi wa umma na wananchi kwa ujumla.

Katika ukaguzi huo, timu ilitembelea miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi katika Kituo cha Afya Hombolo, Shule ya Sekondari Mtemichiloloma, Kituo cha Afya Mkonze na Shule ya Sekondari Bihawana, ambapo ilijionea maendeleo ya utekelezaji wa miradi hiyo na kufanya majadiliano na wasimamizi pamoja na wakandarasi kuhusu hatua zilizofikiwa na changamoto zinazojitokeza.