Na. Asia Singano, na Joseph Mahumi, WF – Dodoma
Ugeni kutoka Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano, Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, umetembelea Jengo jipya la Wizara ya Fedha, lililopo Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma, kwa lengo la kujionea mazingira ya kazi pamoja na kujifunza namna Kitengo cha Mawasiliano Serikalini cha Wizara ya Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kinavyotekeleza majukumu yake ya mawasiliano ya Serikali na utoaji wa taarifa kwa umma.
Katika ziara hiyo, wageni hao walipata fursa ya kutembelea ofisi mbalimbali ndani ya Jengo hilo na kujionea mifumo ya kisasa inayotumika katika utekelezaji wa shughuli za Wizara, hususan katika maeneo ya Ofisi za Viongozi, Kumbi za Mikutano, Ofisi za Utawala, Ofisi ya Mawasiliano Serikalini pamoja na sehemu ya maegesho ya magari.
Ugeni huo kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Wizara ya Fedha na Mipango, Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano, uliwahusisha Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Habari na Uhusiano, Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, Bi. Zuhura Mwalim, Afisa Habari na Uhusiano Msaidizi, Bw. Abubakar Haji, Afisa TEHAMA, Bi. Sahiya Kombo, pamoja na Afisa Habari na Uhusiano, Bi. Hamida Suleiman.
Aidha, msafara huo uliongozwa na Afisa Utumishi Mwandamizi wa Wizara ya Fedha, Bw. Salum Said, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bw. Lucius Mwenda, ambaye alisema kuwa ziara hiyo ni sehemu ya ushirikiano wa Serikali unaolenga kubadilishana uzoefu na kuimarisha utendaji kazi kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar.
Alisema kuwa licha ya wageni hao kuwasili kwa ajili ya mafunzo ya kujifunza namna Kitengo cha Mawasiliano kinavyofanya kazi, Wizara iliona umuhimu wa kuwapa nafasi ya kutembelea Jengo jipya la Wizara ili wajionee mazingira bora ya kazi pamoja na mifumo ya kisasa inayotumika katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali.
“Jengo hili limejengwa katika viwango vya kisasa vinavyowezesha mazingira bora ya utendaji kazi, kuongeza morali kwa watumishi pamoja na kuimarisha ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi,” alisema Bw. Salum.
Kwa upande wao, wageni kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano, walieleza kufurahishwa na mandhari ya Jengo hilo, wakisifu mpangilio wa ofisi, usasa wa mazingira ya kazi pamoja na mifumo mbalimbali inayorahisisha utendaji kazi wa kila siku.
Walisema kuwa mazingira hayo yanawavutia watumishi kupenda kazi, kuongeza ari ya utendaji pamoja na kuchochea uwajibikaji na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.
Katika ziara hiyo, wageni hao waliambatana na Maafisa Habari wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini cha Wizara ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliokuwa wakitoa maelezo kuhusu shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na kitengo hicho katika kuhabarisha umma kuhusu shughuli za Wizara.

