Na Happy Lazaro, Arusha
MAWAKILI 500 kutoka mikoa mbalimbali wamekutana jijini Arusha katika semina na mijadala ya kitaaluma itakayohitimishwa na mkutano mkuu Alhamisi.
Mkutano mkuu utafanyika Alhamisi, ambapo unatarajiwa kufunguliwa na Jaji Mkuu, George Masaju, na utaambatana na shughuli nyingine, zikiwemo vikao vya kikanda vya mawakili.
Akizungumza jijini Arusha ,Meneja wa Programu wa TLS, Kefar Mbogela, amesema wiki ya mkutano mkuu imeanza
ikiambatana na semina mbalimbali zinazolenga kuwajengea uwezo mawakili hao .
Mbogela amesema kuwa,katika mkutano wake mkuu wa mwaka huu watajadili kwa kina wajibu na mchango wa wanasheria katika kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, ikiwa ni sehemu ya wadau muhimu katika maendeleo ya nchi.
“mada zinazowasilishwa ni pamoja na maadili ya uwakili, ubobezi wa kisheria, namna ya kusawazisha maisha ya kazi na binafsi, afya ya akili pamoja na mbinu za uwekezaji kwa mawakili ili kuwaongezea ufanisi wa maisha nje ya taaluma yao.”amesema Mbogela.
“Hii ni wiki ya TLS tuko Arusha kwa ajili ya mkutano mkuu na tumeanza na semina mbalimbali zitakazoendelea hadi Jumatano, ambapo mawakili wanapata nafasi ya kujadili maswala mbalimbali yakiwemo kubadilishana uzoefu pamoja na maswala ya maadili kwa mawakili, na ubobezi wa kisheria na masuala ya uwekezaji,”amesema.
Mbogela amesema kuwa,kauli mbiu ya mwaka huu inalenga kuangazia nafasi ya mwanasheria katika kuelekea Dira ya Taifa 2050, ambapo TLS inalenga kutazama kwa upna namna wanasheria wanavyoweza kuchangia maendeleo ya Taifa.
Amesema mawakili 500 wanashiriki katika shughuli hizo, ambazo pia zinahusisha utoaji wa elimu ya msaada wa kisheria kupitia matawi 21 ya TLS nchini, ikiwa ni sehemu ya mchango wa chama hicho katika maendeleo ya jamii.
Ameongeza kuwa, mbali na mawakili, semina hizo pia zimewashirikisha wadau kutoka kada nyingine kutokana na umuhimu wa mada zinazojadiliwa kuwa na manufaa mapana zaidi
Mmoja wa washiriki katika semina hiyo , amesema mafunzo hayo ni muhimu katika kuwaongezea uelewa na kuwajengea uwezo mawakili, hasa katika kuwahudumia wananchi wanaohitaji msaada wa kisheria.
“Tunapopatiwa semina kama hizi mara kwa mara zinasaidia sana kutukumbusha wajibu wetu na kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wetu wa kila siku.”amesema.





