Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Samwel M. Maneno amesema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imetoa kipaumbele katika kuboresha hali ya afya ya watumishi wa Ofisi, ameyazungumza hayo wakati akifungua mafunzo maalumu ya afya yaliyoandaliwa kwa Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, tarehe 27 Septemba, 2025 Jijini Dodoma.
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ameeleza kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inatambua umuhimu wa Afya bora kwa Watumishi, katika kutekeleza hilo Ofisi imeandaa mafunzo hayo kwa Watumishi ili waweze kufahamu afya zao na kuweza kujikinga na maradhi mbalimbali.
*“Kwa kutambua umuhimu wa afya bora kwa watumishi na ndio nguzo kuu ya uwezo na ufanisi katika utendaji kazi wa kila siku, bila kuwa na afya bora weledi, ubora na uwajibikaji unaotarajiwa hautoweza kufikiwa.”* Amesema Naibu Mwanasheria Mkuu
Aidha, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali amewataka Watumishi kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo kwa kufuatilia mada zitakazowasilishwa na wataalamu wa masuala ya afya ili kupata elimu ya afya na kuwasaidia kuepuka magonjwa mbalimbali na kuwafanya kuwa na afya bora hivyo kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
*“Niwaombe tuzingatie mafunzo haya na elimu tutakayopewa na Wataalamu hapa iwe chachu ya kuboresha Afya zetu na tukiwa na afya bora tutaweza kutekekeleza majukumu yetu kwa ufasaha.”* Amesema Mhe. Maneno.
Awali akimkaribisha Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mkurugenzi wa Divisheni ya Utawala na Rasilimali Watu Bi. Faith Minani ameeleza kuwa mafunzo hayo ya afya kwa Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu yatahusisha masuala ya HIV-AIDS, magonjwa ya Homa ya Ini, na magonjwa ya Afya ya akili.
*“Mafunzo haya yatahusisha kupata elimu wa masuala ya HIV-AIDS, magonjwa ya Homa ya Ini pamoja na Afya ya Akili na baada ya mafunzo haya kutakuwa na zoezi la upimaji wa hiari kwa Watumishi wote.”* Amesema Bi. Faith
Mafunzo hayo kwa Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali yameendeshwa na Wataalamu wa Afya kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, na Hospitali ya Benjamini Mkapa.




