*Atoa wito kwa waokoaji kuzingatia usalama
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, amekutana na kuzungumza na kundi la ndugu wa mafundi waliopatwa na ajali ya kukwama chini ardhi pamoja na kundi la waokoaji wanaoendelea na zoezi la uokoaji katika mgodi wa Nyandolwa.
Katika mkutano huo uliofanyika karibu na eneo la tukio, Mhe. Mboni aliwataka ndugu wa waathirika kutoa maoni, ushauri na mapendekezo kwa uwazi ili Serikali iweze kuona namna bora ya kuwasaidia, hasa katika kipindi hiki kigumu cha majonzi na mashaka.
“Tunataka kusikia kutoka kwenu maoni, ushauri, na mahitaji yenu ili tuweze kuchukua hatua zinazogusa maisha yenu moja kwa moja,” alisema Mboni mbele ya wanandugu na viongozi wa eneo hilo.
Katika hatua ya kusaidia kukabiliana na hali ya maisha ya wahanga, Mboni alieleza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Maafa itatoa huduma ya chakula kwa ndugu wa waathirika, wafanyakazi na waokoaji katika tukio hilo kupitia mtoa huduma wa chakula. Lengo ni kuhakikisha kuwa huduma za msingi zinapatikana kwa wale waliopo katika eneo la tukio, huku juhudi za uokoaji zikiendelea.
“Tusingependa kuona watu wakipata changamoto za mahitaji wakati tayari wana uzunini, hivyo familia za watu 18 ambao bado wapendwa wao hawajaokolewa mchague wawakirishi watatu ambao serikali itawapa mahitaji muhimu kwa muda ambao mtakuwa mkiwasubiri wapendwa wenu,” alisema Mboni.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia usalama wa waokoaji hasa ikizingatiwa kuwa mvua zinaendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo, jambo linaloongeza changamoto katika shughuli za uokoaji.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Mhe. Julius Mtatiro, alitoa pongezi kwa timu za uokoaji kwa kazi kubwa na ya kujitolea wanayoendelea kuifanya katika mazingira magumu. Alitoa wito kwa ndugu na wananchi kuendelea kuwa watulivu na kushirikiana kwa karibu na mamlaka husika wakati wanaendelea na juhudi za kuwaokoa mafundi waliokwama chini ya ardhi.
“Serikali ipo pamoja nanyi katika kipindi hiki. Tuendelee kuwa na subira na mshikamano wakati wataalamu wakiendelea na zoezi la uokoaji,” alisema Mtatiro.
Shughuli za uokoaji zinaendelea kwa tahadhari kubwa, huku timu za waokoaji kutoka taasisi mbalimbali zikiendelea kushirikiana kuhakikisha mafundi walioko chini ya kifusi wanaokolewa.
Mgodi wa Nyandolwa unaomilikiwa na kikundi cha Wachapakazi, Agosti 11, 2025 ulipata ajali ya kutitia kwa ardhi na kupelea kuporomoka kwa kifusi kilichosababisha kuwafunika mafuni 25 waliokuwa wakifanya ukarabati katika maduara matatu tofauti ambapo mpaka sasa mafundi 7 wameshatolewa kutoka kwenye maduara hayo na jitihada za kuwaokoa mafundi 18 waliobaki zinaendelea.