Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwasili katika Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Brazil (Itamaraty Palace) kushiriki Ufunguzi Mkutano wa pili wa Brazil na Afrika kuhusu Usalama wa Chakula, Mapambano dhidi ya Njaa na Maendeleo Vijijini unaofanyika Jijini Brasilia . Tarehe 22 Mei 2025.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akishiriki Ufunguzi wa Mkutano wa pili wa Brazil na Afrika kuhusu Usalama wa Chakula, Mapambano dhidi ya Njaa na Maendeleo Vijijini unaofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Brazil (Itamaraty Palace) Jijini Brasilia . Tarehe 22 Mei 2025.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwa katika picha za pamoja na viongozi mbalimbali mara baada ya Ufunguzi wa Mkutano wa pili wa Brazil na Afrika kuhusu Usalama wa Chakula, Mapambano dhidi ya Njaa na Maendeleo Vijijini unaofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Brazil (Itamaraty Palace) Jijini Brasilia . Tarehe 22 Mei 2025.
……………..
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amewasihi watanzania wanaoishi nchini Brazil kuzingatia sheria za nchi hiyo pamoja na kujihusisha na biashara halali katika nchi hiyo.
Makamu wa Rais amesema hayo alipotembelea Ubalozi wa Tanzania nchini Brazil uliopo Jijini Brasilia na kuzungumza na watumishi wa ubalozi huo ambapo alipokea taarifa ya baadhi ya watanzania kutumikia vifungo mbalimbali katika magereza nchini Brazil. Amemsihi Balozi wa Tanzania nchini Brazil Mhe.Dkt. John Simbachawene kufanya vikao na watanzania waishio Brazil kuwasisitiza kujielekeza zaidi katika fursa nzuri na zitakazotangaza vema Taifa la Tanzania.
Makamu wa Rais amewasihi kuhakikisha wanakuza diplomasia ya uchumi baina ya Tanzania na Brazil kwa kuwa Taifa hilo ni kubwa lenye idadi kubwa ya watu hivyo ina fursa ya masoko kwa bidhaa za Tanzania. Pia amesema nchi hiyo imewekeza vizuri katika sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, utafiti, viwanda pamoja, uchumi wa buluu pamoja na michezo hivyo ni fursa nzuri kushirikiana na Tanzania.
Amewataka kutangaza fursa mbalimbali zilizopo nchini Tanzania pamoja na kuvutia wawekezaji. Pia amewaelekeza kuendelea kutafuta nafasi za masomo kwa watanzania ili waweze kunufaika na uwepo wa teknolojia mbalimbali zilizopo nchini Brazil.
Makamu wa Rais anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa pili wa Brazil na Afrika kuhusu usalama wa chakula, mapambano dhidi ya njaa na maendeleo vijijini unaofanyika Jijini Brasilia.