Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi na hatua za Mpito za haki za kukabiliana nayo kwa njia ya mtandao Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili 2025.
Aidha, katika mkutano huo uliofanyika kwa njia ya mtandao, Mhe. Rais Dkt. Samia amesisitiza umuhimu wa kufanikisha ajenda ya upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa zaidi ya watu milioni 950 wasio na nishati hiyo barani Afrika. Pia amebainisha Mkakati wa Serikali wa kuhakikisha asilimia 80 ya watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Mkutano huo ulioandaliwa na Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Brazil, Mhe. Luiz Inacio Lula Da Silva na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe. Antonio Guterres ulihudhuriwa na Wakuu wa Nchi na Serikali kutoka Mataifa 17 duniani, pamoja na Wenyeviti wa Mikutano ya Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (UNFCCC) iliyofanyika mwaka 2023 (Umoja wa Falme za Kiarabu), 2024 (Azerbaijan) na utakaofanyika Belem, Brazil mwezi Novemba 2025.