Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar, Mhe. Omar Said Shaaban amewasili jijini Harare, Zimbabwe kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Kawaida wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) utakaofanyika jijini hapa kuanzia tarehe 12 hadi 14 Machi 2025.
Mara baada ya kuwasili, Mhe. Waziri Shaaban amepokelewa na Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Inspekta Jenerali wa Polisi Mstaafu, Mhe. Simon Sirro aliyekuwa ameongoza na na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Said Shaibu Mussa.
Waziri Shaaban anatarajiwa kuongoza ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano huo wa Baraza la Mawaziri ambao ulitanguliwa na vikao vya Kamati ya Makatibu Wakuu bna Wataalam tarehe 3 hadi 5 Machi, 2025; Kamati ya Kudumu ya Makatibu Wakuu, tarehe 6 na 7 Machi, 2025; na Kamati ya Fedha, tarehe 9 na 10 Machi, 2025.
Viongozi wengine waliopo kwenye ujumbe wa Tanzania ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Bi Amina Khamis Shaaban, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Bw. Suleiman Hassan Serera, Mratibu waTanzania masuala ya SADC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri na Maafisa Waandamizi kutoka Serikalini.