FARIDA MANGUBE, MOROGORO
Chama cha Wafanyakazi wa Reli Tanzania (TRAWU) kimempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa jitihada za kuboresha mashirika ya TRC na TAZARA, huku kikiomba uingiliaji wake katika changamoto ya kutosainiwa kwa Mkataba wa Hali Bora kwa wafanyakazi wa TRC.
Akizungumza mkoani Morogoro baada ya kikao cha baraza kuu la TRAWU, Katibu Mkuu wa chama hicho, Juma Masoud, alisema changamoto nyingi zinazowakabili wafanyakazi wa TRC na TAZARA bado hazijapatiwa ufumbuzi na menejimenti.
Kwa upande wa TAZARA, Masoud alieleza kuwa serikali imefanikiwa kulipa mishahara ya wafanyakazi, kuboresha miundombinu ya reli pamoja na kuendelea kutafuta mwekezaji wa kuimarisha shirika hilo.
Hata hivyo, alisema mishahara ya wafanyakazi wa TAZARA kwa Februari 2025 haijalipwa, akidai kuna uzembe wa menejimenti katika kukusanya madeni kutoka kwa wawekezaji wanaotumia reli hiyo kupitia ada ya “Open Access Fee.”
Kwa TRC, Masoud alipongeza serikali kwa kukarabati reli ya zamani ya MGR, kupandisha mishahara, kulipa madeni sugu ya wafanyakazi, na kufufua safari za treni, ikiwa ni pamoja na uzinduzi wa treni za umeme (EMU). Pia alieleza kuwa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) umeongeza ajira kwa vijana.
Pia , alieleza kuwa licha ya kuwepo kwa rasimu ya Mkataba wa Hali Bora kwa wafanyakazi wa TRC, menejimenti ya shirika hilo imesita kuusaini kwa zaidi ya miaka miwili sasa mkataba huo.
Mwenyekiti wa TRAWU Taifa, Jacob Shindika, alidai kuwa chama kinakumbana na vikwazo katika kutekeleza majukumu yake ndani ya TRC, huku viongozi wake wakitishiwa na kudhalilishwa. Pia alihofia kuwa huenda kuna njama za kuanzisha chama kingine cha wafanyakazi kinacholinda maslahi ya menejimenti badala ya wafanyakazi.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Wanawake wa TRAWU, Froida Mwakatundu, alisema wafanyakazi wa TRC wanakabiliwa na changamoto kubwa ya mafao duni, ambapo hata baada ya kutumikia shirika kwa zaidi ya miaka 40, wanapokea kiinua mgongo cha shilingi milioni moja pekee.
Kutokana na changamoto hizo, TRAWU imemuomba Rais Samia kuingilia kati ili kuleta suluhisho, ikiamini kuwa yeye ni kiongozi msikivu