Katika jitihada za kuimarisha uwezo wa utoaji wa huduma za dharura wakati wa mlipuko wa Ugonjwa wa Marburg, Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Chama cha Madaktari wa Magonjwa ya Dharura Tanzania (EMAT) imeendesha mafunzo maalum kwa watumishi wa afya waliopo mstari wa mbele katika Hospitali ya Wilaya ya Biharamulo.
Mafunzo haya ya siku tano yamehusisha watumishi waliopo kwenye kambi ya Marburg, wakipewa elimu ya kina, ujuzi wa kitabibu, na mbinu za kisasa za utambuzi, matibabu, na udhibiti wa maambukizi ya ugonjwa huu hatari. Lengo kuu la mafunzo haya ni kuhakikisha watumishi wa afya wanaimarisha utayari wa kukabiliana na dharura zinazotokana na Marburg na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wagonjwa au wanaohisiwa kuwa na maambukizi.
Akizungumza wakati wa hafla ya kufunga mafunzo hayo, Mkuu wa Timu ya Matibabu, Dkt. Michael Kiremeji, alieleza kuwa mafunzo haya ni nyenzo muhimu katika juhudi za kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo.
“Mafunzo haya yanalenga kuhakikisha wahudumu wa afya wanakuwa na ujuzi wa hali ya juu wa kushughulikia wagonjwa wa Marburg kwa haraka, kupunguza hatari ya maambukizi katika vituo vya afya, na kulinda jamii dhidi ya mlipuko wa ugonjwa huu,” alisema Dkt. Kiremeji.
Serikali inaendelea kuwekeza katika ujenzi wa mifumo madhubuti ya udhibiti wa magonjwa ya mlipuko, ikiwemo kutoa mafunzo kwa watumishi wa afya, kuimarisha upatikanaji wa vifaa tiba, na kuelimisha jamii kuhusu tahadhari dhidi ya Marburg.