Na Sophia Kingimali.
Rais Dkt Samia Suluhu Hassan anatarajia kuanza kukutana na wananchi na kusikiliza kero zao lengo likiwa ni kumuenzi kwa vitendo Hayati Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi ambae alikuwa akifanya hivyo kipindi cha uongozi wake lakini pia kujua utendaji kazi wa watendaji wake katika kuwahudumia wananchi.
Hayo ameyasema leo Machi 5,2024 Katibu wa Itikadi,Uenezi na Mafunzo Paul Makonda jijini Dar es salaam wakati akitoa taarifa fupi kuhusu ziara yake katika mikoa 23 ya Tanzania Bara.
Amesema Rais Dkt Samia atumia siku moja ya kila mwezi kukutana na wananchi katika ofisi za CCM mkoa wa Dar es salaam,Dodoma na Zanzibar.
“Rais amepanga kutenga siku moja kwa kila mwezi ili kuwasikiliza wananchi wake bila kujali itikadi,dini wala ukabila sasa hapa nitumie salama kwa watumishi ambao wananchi walishaleta kero zao na ukuzitatua aje azifikieshe kwa Rais hapo kiama kitakua mlangoni kwako”,Amesema Makonda.
Akizungumzia ziara yake amesema kuna mambo mbalimbali yaliyobainika kwenye ziara hiyo ambayo yatakabidhiwa kwa katibu mkuu wa chama ambapo mengine yalishughulikiwa papo hapo.
Amesema kati ya mambo yaliyobainika ni Dhuruma kwani watanzania wengi wameumizwa na dhuruma ambayo imegawanyikwa kwenye mambo mengi.
“Sisi kama chama tunajukumu la kuishauri serikali ili kupambana na dhuruma hiyo ili kuwasaidia wananchi”Amesema Makonda.
Akitaja maeneo yaliyokithiri kwenye dhuruma amesema ardhi imekuwa changamoto wananchi wengi wamedhulimiwa ardhi zao ambapo walimuamba waziri wa ardhi kwenda kushughulikia na tayari hatua mbalimbali zimechukuliwa ili kutoa funzo kwa watu wanaotumia pesa kutapeli ardhi za waonyonge.
Amesema Waziri anapaswa kufanya mapitio kwa watendaji wote ambao wameweka minyororo ya utapeli wa ardhi aweze kuwachukulia hatua kwani utapeli wa ardhi umeonekana kuwa na mtandao mpana na si wa mtu mmoja pekee.
“Kazi anayoifanya waziri wetu wa ardhi inapaswa kuungwa mkono na watendaji wote na wale wanaohusika na utapeli wachukuliwe hatua ili kukata minyororo hiyo ya utapeli”Amesema.
Ameongeza kuwa Kila mtendaji ambae amekuwa katika mnyororo wa kuwaonea wananchi wabainishwe na wachukuliwe hatua stahiki ili kuleta mabadiliko chanya kwa wananchi.
Aidha Amesema kuwa zipo dhuruma nyingi zilizofanyika hasa za watu kujipatia mali kiudanganyifu hivyo mamlaka husiki zinapaswa kuchukua hatua ili kukomesha dhuruma hizo.
Amesema tatizo lingine ni viongozi kutokutatua kero za wananchi ambazo huwa wanazisikiliza hivyo chama kinaelekeza kila alie na nafasi anapaswa kutatua kero za wananchi kwani ofisi aliyopo ni ya umma hivyo kutokutatua kero zao ni kinyume na utumishi.
“Viongozi tusitatue changamoto za wananchi kwa sababu ya kujuana bali tutatue changamoto kwani wanahaki ndani ya serikali ya Jamuhuri ya Muungano”Ameongeza.
Aidha changamoto nyingine waliokutana nayo ni ukatili wa kijinsia ambao unejitokeza kwenye baadhi ya mikoa hivyo changamoto hiyo inashughulikiwa ili kuja mkakati thabiti wa kuzuia ukatili huo.
Sambamba na hayo amesema ziara hiyo imekuwa na mafanikio makubwa sana na kuwapongeza viongozi wote wa chama walioshirikiana katika ziara hiyo kwenye mikoa yao wakiwemo wenyeviti,waNEC na wengine ambapo kazi hiyo ilikuwa ni utekelezaji wa ilani ya chama ndani ya chama na nje ya chama.