Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya ndani ya Nchi Kaspar Mmuya akizungumza wakati wa ufunguzi wa Baraza dogo la wafanyakazi wa Jeshi la Zimamoto lililofanyika Jijini Mwanza ![]()
![](https://fullshangweblog.co.tz/wp-content/uploads/2023/12/IMG-20231219-WA0133-1024x563.jpg)
Wanachama wa Baraza dogo la wafanyakazi wa Jeshi la Zimamoto wakiwa kwenye picha ya pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya ndani ya Nchi Kaspar Mmuya (katikati kwa waliokaa)
![](https://fullshangweblog.co.tz/wp-content/uploads/2023/12/IMG-20231219-WA0134-1024x507.jpg)
Viongozi mbalimbali waliohudhuria Baraza la wafanyakazi wa Jeshi la zimamoto na uokoaji ![]()
![](https://fullshangweblog.co.tz/wp-content/uploads/2023/12/IMG-20231219-WA0135-1024x682.jpg)
Wanachama wa Baraza la wafanyakazi wa Jeshi la Zimamoto wakiwa ukumbini
………………………..
Na Hellen Mtereko, Mwanza
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya ndani ya Nchi Kaspar Mmuya, amelitaka Jeshi la Zimamoto nchini kudhibiti matumizi ya fedha za miradi zinazotolewa na Serikali hatua itakayosaidia kufanikisha utekelezaji wa miradi hiyo muhimu.
Rai hiyo ameitoa leo Jumanne Desemba 19, 2023 kwenye mkutano wa ufunguzi wa Baraza dogo la wafanyakazi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji uliofanyika katika ukumbi wa Benki kuu Jijini Mwanza.
Amesema fedha inayotolewa kwaajili ya miradi ikitumika kwa madhumuni yaliyopangwa itachochea kuharakisha utekelezaji wa shughuli za maendeleo na miradi itakuwa na tija kubwa kwenye jamii.
Aidha, amelipongeza Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kuendelea kutoa huduma katika maeneo mbalimbali hapa nchini sambamba na kutekeleza mpango wa kujengea uwezo wananchi ili wawe na utayari wa kuongeza nguvu katika shughuli za uzimaji moto na Uokoaji.
Akizungumza kwenye Mkutano huo Kamishina Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji John Masunga, amesema mwaka wa fedha 2023/2024 Jeshi hilo limetengewa Bilioni 9.9 kwaajili ya utekelezaji wa miradi ya upanuzi na uboreshaji wa huduma za Zimamoto na Uokoaji ikiwemo ununuzi wa magari matano ya kuzimamoto na uokoaji, uendelezaji wa ujenzi wa vituo saba vya Zimamoto na Uokoaji katika Mikoa ya Songwe,Simiyu,Kagera,Njombe, Manyara,Katavi na Geita.
Akizungumza hali ya upatikanaji wa huduma za Zimamoto na Uokoaji nchini Masunga amesema, Jeshi hilo lina jumla ya vituo 82 vya Zimamoto na Uokoaji katika Mikoa yote Tanzania Bara, kati ya vituo hivyo 56 vipo katika ngazi ya Wilaya na 26 kwenye viwanja vya ndege.
“Jeshi lina Ofisi 41 za kutoa elimu ya Kinga na tahadhari ya majanga ya moto katika Wilaya mbalimbali na vituo saba vya kutoa huduma mipakani (OSBPs),pia Jeshi linauhitaji wa vituo vipya 175 katika Wilaya na maeneo mengine ili kusigeza huduma karibu zaidi na wananchi”, amesema Masunga
Masunga amesema Jeshi hilo linakabiliwa na changamoto ya uhaba wa vifaa na vitendea kazi kwaajili ya utoaji wa huduma,uchache wa vituo vya Zimamoto na Uokoaji nchini, ujenzi holela katika maeneo mengi hasa mijini unaosababisha Askari kutokufika kwa urahisi wakati wa dharula za moto na majanga mengine pamoja na uchache wa maafisa na Askari kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya Jeshi.
Kwaupande wake Mrakibu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mwanza Kamila Labani, amesema licha ya kuwepo na baadhi ya wananchi kutokutoa taarifa kwa wakati pindi majanga yanapotokea wanaendelea kufanya kazi kwa weledi mkubwa katika kuhakikisha Mkoa unakuwa salama.
“Wanaotoa taarifa kwa wakati inatusaidia sisi Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kufika haraka kwenye tukio na madhara yanakuwa siyo makubwa ukilinganisha na tunavyopata taarifa kwakuchelewa”, amesema Labani
Awali akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Amos Makalla Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Amina Makilagi amesema, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linafanya kazi ya kutukuka ya kuokoa watu na mali zao pindi majanga yanapotokea.