Mwenyekiti wa Kijiji cha Kamasi,Tatu Warioba, akipata chanjo ya Uviko-19 kutoka kwa muuguzi baada ya kupata elimu inayotolewa na wataalamu wa fya wilayani Ukerewe.Picha na Baltazar Mashaka.
Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Kanali.Denis Mwila, akihamasisha wananchi wa Kisiwa cha Gana, kujitokeza kupata chanjo ya Covid-19.

…………………………………………………………….

NA BALTAZAR MASHAKA, UKEREWE

WANANCHI wa Kitongoji cha Kisiwa cha Gana,Kijiji cha Kamasi,Kata ya Ilangala, Wilaya ya Ukerewe, wajitokeza kwa wingi kupata elimu ya chanjo ya Uviko-19 iliyotolewa na timu ya wataalamu wa Afya wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Kanali. Denis Mwila.  

Akizunguma na wananchi hao jana, Kanali Mwila, aliwataka na kuwasihi wananchi wa kata hiyo kutumia fursa hiyo kujitokeza kuchanja kwa manufaa ya afya zao, kujikinga wao binafsi na kuwalinda wengine na kiuchumi.
Pia alitahadharisha kuwa siku mtu maradhi yakimpata, gharama zitakazotumika kumtibu ni kubwa sana na hivyo kusababisha kutumia fedha nyingi lakini pia maradhi hayo yanasababisha vifo na kupoteza nguvu kazi ya jamii na taifa.

“Eneo hili la Gana lina muingiliano mkubwa wa watu kutokana na shughuli za kiuchumi, ili kuwa salama na Uviko-19 ni vizuri kuchanja na chanjo zipo za kutosha, ni salama na hazia madhara, ukiachilia mbali maudhi madogo madogo,”alisema Kanali Mwila. 

Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Dk.Getera Nyangi,akitoa elimu ya ugonjwa wa Uviko-19  aliwatoa hofu wananchi hao na kuwataka kupuuza maneno yasiyo kuwa na uthibitisho juu ya chanjo hiyo ambayo imethibitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) na Wizara ya Afya. 

Aliyataja makundi na watu wenye sifa za kupata chanjo hiyo ni pamoja na wenye umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea na sio kwa watu wenye umri mkubwa tu kwa sababu ugonjwa hauchagui.

“Hadi sasa takribani watu 2,064 wilayani Ukerewe na hakuna hata mmoja aliyeripoti kupata changamoto yoyote ya kiafya inayotokana na chanjo, hivyo tuchanje kwa afya zetu,” alisema Dk. Nyangi. 

Aidha wananchi wa kitongoji cha Gana waliojitokeza kwa wingi kuchanja walipata fursa ya kuuliza maswali yanayowatatiza na kupatiwa majibu ya kitaalamu. 

Baadhi walisema kuwa baada ya kupata elimu hiyo na kupata uelewa kuhusu ugonjwa wa uviko-19 kutoka kwa wataalamu, wako tayari na wataendelea kuhamasishana wakachanje bila shuruti ili kulinda afya zao.