Na Silvia Mchuruza.Bukoba.
KUTOKANA na ongozeko la abiria wa usafiri wa anga mkoani Kagera, Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) limeongeza ndege ya pili ili kukabiliana na kiwango cha abiria mkoani humo.
Mtendaji Mkuu wa ATCL, Mhadisi Ladisraus Matindi amesema kuwa Mkoa wa Kagera una zaidi ya abiria 2,400 kila mwezi sawa na asilimia 70 za ujazo wa ndege kwenda na kurudi
Matindi ameyasema hayo leo mkoani Kagera alipofanya ziara ya kawaida ya kikazi kwa ajili ya kuongea na wadau wa shirika hilo na kuongeza kuwa katika kipindi cha msimu wa sikukuu, ATCL imelazimika kuleta ndege mbili ili kumudu wingi wa abiria.
Amesema licha ya kuongeza ndege ya pili ambapo zote zinafanya kazi kila siku lakini kwa mujibu wa Meneja wa uwanja wa ndege wa Bukoba, ni kwamba ndege zote zimejaa hadi Januari 15.
Pia Matindi ametolea ufafanuzi wa malalamiko ambayo yamekuwepo kwa abiria wa usafiri huo kuhusu mizigo yao kukwama uwanja wa ndege kuwa na changamoto hiyo inatokana na uwanja wa ndege wa Bukoba kuwa mfupi.
Matindi alisema changamoto ya uwanja huo wa ndege inaendelea kutatuliwa ili ziweze kutua ndege kubwa
Naye Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Brigedia Jenerali Marco Gaguti amewaomba wakazi wa Mkoa wa Kagera kutumia usafiri wa anga kiuchumi zaidi ili kukuza uchumi wa nchi na mkoa na hata kwa wananchi wenyewe kutokana na kuzalisha bidhaa mbalimbali ambazo zinaweza kusafirishwa nje ya mkoa pia.
“Tumeshaanza hatua za awali za kupanua uwanja huo na kutokana na mahitajio ya wateja Mkoa utaweka msukumo ili upanuzi uende kwa haraka ambapo upanuzi huo utaenda sambamba na kuweka taa ili kusaidia ndege kutua wakati wa mawingu na usiku” alisema Gaguti.