Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh.Ummy Mwalimu akizungumza na Wanahabari mara baada ya kutembelea ofisi za TMDA kukabidhi Magari 61 ambayo yataenda kurahisisha huduma ya chanjo kwa baadhi ya halmashauri nchini.Mkurugenzi wa Kinga Dk.Leonard Subu akiongea na Wanahabari leo katika ofisi za TMDA Jijini Dar es Salaam
Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh.Ummy Mwalimu akikata utepe kukabidhi magari 61 ambayo yataenda kurahisisha huduma ya chanjo kwa baadhi ya halmashauri nchini.
**********************
NA EMMANUEL MBATILO
Wananchi wametakiwa kuhudhulia katika vituo vya huduma ya Afya Septemba 26 hadi 30 mwaka huu kwani kutakuwa na uzinduzi wa kampeni ya chanjo ya Rubella na surua kwa nchi nzima iliandaliwa na Wizara hiyo.
Ameyasema hayo leo Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh.Ummy Mwalimu alipotembelea ofisi za TMDA kukabidhi magari 61 ambayo yataenda kurahisisha huduma ya chanjo kwa baadhi ya halmashauri nchini.
“Wazazi na walezi ni vyema mkajitokeza siku hiyo kwa kumpeleka mtoto kupata chanjo kwani chanjo ya Rubella inaenda kumsaidia kuepukana na magonjwa ya moyo na itatolewa nchi nzima”alisema
Akizungumza na Wanahabari Jijini Dar es Salaam, Mh.Ummy amewahakikishia watanzania kuwa Serikali imejipanga kuboresha huduma ya chanjo kulingana na Maendeleo ya Sayansi na Teknolojia.
“Serikali imekuwa ikijitaidi kuhakikisha huduma za chanjo zinawafikia watu wote ndiyo maana imekuwa ikitolewa billion 30 kila mwaka ili kufikisha huduma hii kwa wananchi wote”alisema
Pia alisema magari hayo ni kwaajili ya kuimarisha na kurahishisha huduma ya utoaji na upatikanaji wa chanjo kwa nchi nzima.
Aidha amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri zote kuyakatia bima magari hayo ili kuiepushia Serikali hasara ya mabilioni ya fedha ambayo imekuwa ikitumia kwa ajili ya ununuzi wa magari mapya.
Alisema Tanzania imekuwa ikijitahidi kutoa huduma bora kwenye masuala ya chanjo na imefanikiwa kushika nafasi ya tatu kwa bara la Afrika.
Aliongeza kwa sasa nchi inatoa chanjo 9 na chanjo hizo ni kwa ajili ya watoto, ambapo 8 ni kwaajili ya watoto chini ya umri wa miaka miwili na hiyo moja ni chanjo ya Mlango wa kizazi ambayo inatolewa kwa wasichana wenye miaka 9 hadi 14.
Alisema chanjo hizo zinakinga magonjwa 13 yakiwemo Kifua kikuu, Kifadulo, Ndonda, Koo Pepo punda na homa ya Inni.
Pia alisema kwa mwananchi aliyezaliwa Tanzania kuanzia 2002 kwenda chini ndiye anayetakiwa kupata chanjo ya homa ya inni.
“Katika bajeti kipaumbele changu cha kwanza ni chanjo kwani kinga ni bora kulikoni tiba hivyo ni vizuri wananchi mkajitokeza kwenye masuala ya chanjo”alisema
Katika hatua nyingine amewataka wananchi kutambua chanjo ya mlango wa kizazi haina madhara yoyote kwa mtoto hivyo ni vyema wazazi wakawapeleka Watoto kupata Chanjo hiyo.
“Mpaka Sasa wameshatoa chanjo ya kwanza ya mlango wa kizazi kwa wasichana kwa asilimia 67 na ya pili 50 hivyo wazazi ni vyema mkawaleta mabinti kupata chanjo hii”alisema
Mkurugenzi wa Kinga Dk.Leonard Subi alisema chanjo ni jambo la muhimu na linaloaminika kwani inaenda kuibua kinga za mwili.
“Katika hotuba yako Waziri ulisema wewe sio Waziri wa magonjwa bali ni wa afya na ni lazima tuwe na watu wenye afya bora watakaochangia pato la taifa”alisema
Alisema uhitaji wa magari ni mkubwa sana na serikali imekuwa ikijitahidi kuweza kutatua kero hiyo kwani magari hayo yaliyonunuliwa yataenda kurahisisha upatikanaji wa huduma ya chanjo.
Naye Meneja Mpango Taifa wa Chanjo,Dkt.Dafrosa Lyimo alisema magari hayo yatakwenda kurahisisha huduma ya chanjo katika Halmashauri mbalimbali nchini.
“Tumekuwa tukijitahidi kutoa huduma ya chanjo kwa jamii ili kuweza kuondoa changamoto mbalimbali za magonjwa ambayo yanaweza kuzuilika”alisema Dkt.Dafrosa.