Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe (Mwenye suti ya bluu) akisalimiana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama mara baada ya kuwasili kwa ajili ya ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi katika jengo la tatu la abiria (TB III) katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jioni ya leo.Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe katikati akiwa anaelekea katika jengo la tatu la Abiria (TB III) kuona maendeleo ya mradi wa ujenzi, kulia kwake ni Mhandisi Msimamizi wa Ujenzi wa jengo hilo Barton Komba na kushoto kwake ni Msimamizi wa miradi ya Viwanja vyote vya Ndege Tanzania Mhandisi Godson Ngomuo.Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe akisikiliza maelezo kutoka kwa Mhandisi Msimamizi wa Ujenzi Barton Komba kutoka Wakala wa barabara (TANROADS) alienyoosha mkono juu kuhusu eneo la maegesho ya magari katika Jengo la tatu la Abiria (TB III) wakati wa ziara yake Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jioni ya leo.Mhandisi msimamizi wa Ujenzi wa jengo la tatu (TB III) la abiria Barton Komba akitoa maelezo juu ya Mradi wa jengo hilo kwa Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe (wa kwanza kushoto), katikati ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama.Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe katikati akiwa amekaa katika moja ya kiti kilichofungwa katika sehemu ya abiria wanaoondoka katika jengo la tatu la abiria (TB III) katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jioni ya leo.Viti vilivyofungwa katika eneo la kuondoka abiria katika jengo la tatu la abiria Kiwanja Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA).
…………………..
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe ameweka wazi kwamba baada ya siku tisa Jengo la Tatu la abiria (TB III) katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) litakabidhiwa rasmi kwa Wakala wa Barabara (TANROADS) na kisha kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA).
Waziri Kamwelwe amebainisha hayo leo alipokuwa katika ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo.
“Kwa ujumla mifumo mingi ya jengo hili imekamilika na kama kama mnavyoona sehemu nyingi zimeandikwa namba tisa (9) hiyo ina maana kwamba zimebaki siku tisa na kwa maana hiyo tarehe 29 Mei 2019 mkandarasi atakabidhi rasmi jengo”.
Awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa TB III, Kaimu Mkurugenzi Mkuu TANROADS Mhandisi Crispin Akoo alibainisha kwamba
kutokana maendeleo mazuri ya ujenzi Mkandarasi anatarajia kukabidhi jengo siku mbili kabla ya muda wa kwenye mkataba.
“Hadi kufikia terehe 31 Julai 2018 maendeleo yalikua ni asilimia 78.33 lakini hadi kufikia tarehe 18 Mei 2019 ujenzi wote ulikua umefikia asilimia 99.5”.
Kuhusu maandalizi ya uendeshaji Mkurugenzi Mkuu wa TAA Mhandisi Julius Ndyamukama alimweleza Waziri kwamba majaribio na maandalizi ya uendeshaji yalianza tangu mwezi machi mwaka 2018 na yapo katika hatua za mwisho.
“Majaribio ya kwanza ya kwanza ya mifumo na vifaa vinavyotumia umeme yalianza mwezi Julai 2018 kwa sasa yamefikia asilimia 96 na muda sio mrefu yatakamilika”.
Aidha Mhandisi Ndyamukama aliongeza kwamba majaribio hayo yanatarajiwa kufanyika ndani ya miezi mitatu kuanzia mwezi Mei na ifikapo mwezi Agosti yatakua yamekamilika.
Kwa ujumla mradi umeajiri wafanyakazi 1,179 ambapo asilimia 80 ni watanzania na asilimia 20 ni wafanyakazi wa kigeni.