Kaimu Mkuu wa kanda ya Kati Dodoma ,Salome Emanuel akitoa elimu kwa wananchi mbalimbali waliotembelea banda la Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika maonesho ya wakulima maarufu kama nane nane yanayofanyika viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma.
Kaimu Mkuu wa kanda ya Kati Dodoma ,Salome Emanuel akimsikiliza Mwanafunzi kutoka shule ya Sekondari Mkonze,Eva John ambaye alitembelea banda la Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika maonesho ya wakulima maarufu kama nane nane yanayofanyika viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma.
Afisa Masoko TBS,Mussa Luhombero akigawa vipeperushi kwa wananchi ambao waliotembelea banda la Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika maonesho ya wakulima maarufu kama nane nane yanayofanyika viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma.
Wananchi wakiwa kwenye banda la Shirika la Viwango Tanzania (TBS) wakiendelea kupatiwa Elimu katika maonesho ya wakulima maarufu kama nane nane yanayofanyika viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma.
…………………………………………………………..
Na Alex Sonna,Dodoma
Shirika la Viwango Tanzania(TBS), Kanda ya Kati limesema halitasita kuwachukulia hatua za kisheria wauzaji wote wa bidhaa kwenye maduka mbalimbali ambao hawajasajili majengo yao.
Kauli hiyo imetolewa leo na Kaimu Mkuu wa kanda ya Kati Dodoma ,Salome Emanuel katika maonesho ya wakulima maarufu kama nane nane yanayofanyika viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma.
Amebainisha kuwa Shirika hilo lina jukumu kusajili majengo hayo na bidhaa zinazotoka nje ya nchini, ambalo limekasimiwa kwa mujibu wa Sheria ya Fedha namba 8 ya mwaka 2019.
“Shirika linafanya ukaguzi na usajili wa majengo hayo kupitia mifumo rahisi, ambapo muombaji anatakiwa kufanya maombi ya kupata usajili huo kupitia mifumo yetu na anapatiwa namba kwa ajili ya kufanya malipo na baadaye tathmini inafanyika na jengo linasajiliwa,”amesema.
Mkuu huyo amesema ni muhimu wafanyabiashara hao wakasajili majengo yao kwa kuwa kinyume na hapo sheria zitachukuliwa.
“Pia wanaoingiza bidhaa tunawashauri wafanye usajili wa bidhaa zao ili kuepuka kukutana na faini mbalimbali kwa kutokufuata na kuzingatia sheria,”amesema.
Amefafanua kuwa Shirika hilo limepewa majukumu yake kwa mujibu wa sheria namba 2 ya viwango ya mwaka 2019 na linafanya utekelezaji wa majukumu mbalimbali ikiwemo utengenezaji wa viwango.
“Pia utekelezaji katika mifumo mbalimbali ambayo imewekwa scheme ya uthibiti ubora pamoja na uthibitishaji wa ubora wa bidhaa, pia inafanya utekelezaji wa upimaji wa sampuli mbalimbali na uhakiki wa ubora wa vipimo vinavyotumika,”amesema.
Kadhalika, amesema Shirika hilo linatoa elimu kwa umma kupitia mifumo mbalimbali ambayo imewekwa katika kuhakikisha wazalishaji wanapata elimu bora ya uzalishaji wa bidhaa zao kwa kufuata mifumo bora ya uzalishaji.