Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Deus Sangu (pichani), akiwahutubia wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (TALGWU) jijini Dodoma leo, Septemba 17, 2026.

Mhe. Sangu amewapongeza wajumbe hao kwa kuendesha uchaguzi mkuu kwa amani na utulivu, huku akiwasihi viongozi wote waliochaguliwa kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa sheria za nchi na kuendeleza mshikamano imara na Serikali ya Awamu ya Sita.

 Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (TALGWU), Tumaini Nyamhokya, ameishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Mahusiano) kwa mchango wake katika kusimamia uchaguzi wa chama hicho, huku akiahidi kuendeleza ushirikiano madhubuti na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) ili kuleta tija na ufanisi kwa wanachama. Nyamhokya ameyasema hayo leo, Septemba 17, 2026, jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa TALGWU, ambapo alisisitiza msukumo wa kulinda maslahi ya wafanyakazi kote nchini. (Habari na Picha na OWM- KAM)

Sehemu ya wajumbe wa mkutano Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (TALGWU) wakiwa kwenye ukumbi wa mikutano Hotel ya St. Gaspar Dodoma leo Septemba 17,2026.

………..

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu, amekitaka Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU) kuendesha uchaguzi wake kwa kuzingatia Katiba, demokrasia, uwazi, haki, usawa na amani.

Mhe. Sangu ameyasema hayo, leo Septemba 17, 2026, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa TALGWU katika Ukumbi wa St. Gaspar jijini Dodoma, akisisitiza kuwa uchaguzi huo uwe fursa ya kuimarisha umoja na mshikamano badala ya kuwa chanzo cha mgawanyiko.

“Uchaguzi usiwe chanzo cha mgawanyiko, bali uwe fursa ya kuimarisha umoja na mshikamano. Baada ya matokeo kutangazwa, viongozi na wanachama wote wanapaswa kuendelea kushirikiana, kwa kutambua kwamba TALGWU ni kubwa kuliko mtu mmoja,” amesema Mhe. Sangu.

Amesema Serikali inatambua na kuheshimu uhuru wa vyama vya wafanyakazi na itaendelea kushirikiana navyo kupitia mfumo wa majadiliano ya pamoja katika kushughulikia changamoto na masuala ya maslahi ya wafanyakazi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TALGWU Taifa, Ndugu Tumaini Peter Nyamhokya, amesema viongozi wa Chama hicho wamejipanga kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kwa amani na utulivu, huku wakiahidi kuendelea kushirikiana na Chama cha Wafanyakazi Tanzania (TUCTA).

“Tunaishukuru Ofisi yako jinsi ilivyosimama nasi kwenye chaguzi za mikoa zikamalizika salama na kwa amani. Basi na huu wa Taifa pia, nikuhakikishie Mhe. Sangu, utamalizika vizuri,” amesema Ndugu Nyamhokya.