Dar es Salaam
Zaidi ya wananchi 470 wamepatiwa Hatimiliki katika banda la Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakati wa Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
Akizungumza leo, Julai 5, 2026, baada ya kutembelea banda la Wizara hiyo, Dkt. Akwilapo amesema Serikali imepeleka huduma zote muhimu za sekta ya ardhi katika maonesho hayo ili wananchi wapate huduma kwa haraka na kwa urahisi.
Amesema wananchi wanapaswa kutumia kikamilifu fursa ya maonesho hayo kwa kufika katika banda la Wizara ya Ardhi kupata hati miliki za ardhi, elimu kuhusu urasimishaji wa makazi, pamoja na ufumbuzi wa changamoto mbalimbali zinazohusu ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi.
“Maonesho haya ni fursa muhimu kwa wananchi kupata huduma zote za sekta ya ardhi katika eneo moja. Wataalamu wetu wote wapo hapa kuwahudumia. Hivyo, nawasihi wananchi wajitokeze kwa wingi kupata huduma na elimu mbalimbali zinazotolewa” amesema Dkt. Akwilapo.
Aidha, Waziri huyo amewataka wataalamu wa Wizara ya Ardhi wanaotoa huduma katika maonesho hayo kuhakikisha wanatoa huduma kwa ufanisi, weledi na ubora, huku wakizingatia maslahi ya wananchi ili kuongeza imani ya umma katika huduma za Serikali.
Hadi sasa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imehudimia Zaidi ya wananchi 700 katika maonesho hayo na inaendelea kutoa huduma mbalimbali za sekta ya Ardhi ikiwemo ugawaji wa hati miliki, ushauri wa kitaalamu kuhusu masuala ya ardhi, urasimishaji wa makazi, pamoja na kushughulikia changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi katika sekta hiyo.

