Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amesema Serikali kupitia Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) imeendelea kuimarisha sekta ya miundombinu nchini kwa kufanikisha ujenzi wa barabara na madaraja katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026 chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.
Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma leo Mei 20, 2026, Ulega amesema Serikali imefanikiwa kujenga barabara za kitaifa kwa kiwango cha lami zenye urefu wa kilometa 243.13 pamoja na kufanya ukarabati wa kilometa 94.36 kwa kiwango cha changarawe.
Ulega amesema mtandao wa barabara za kitaifa unaosimamiwa na Wizara ya Ujenzi kupitia TANROADS una jumla ya kilometa 37,734.41 ambapo kilometa 12,225.26 tayari zimejengwa kwa kiwango cha lami.
Amefafanua kuwa wakati Tanzania inapata uhuru mwaka 1961, mtandao wa barabara za lami ulikuwa na urefu wa kilometa 1,360 pekee, huku kuanzia Awamu ya Kwanza hadi ya Tano zikijengwa kilometa 9,369.81. Aidha, Serikali ya Awamu ya Sita imefanikiwa kujenga kilometa 1,495.45 za barabara pamoja na madaraja makubwa 18 ndani ya miaka mitano.
“Kwa hakika haya ni mafanikio makubwa yaliyopatikana ndani ya muda mfupi kwa upande wa miundombinu ya barabara na madaraja,” amesema Ulega.
Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema Serikali imekamilisha ujenzi wa madaraja makubwa tisa huku ujenzi wa madaraja 11 ukiendelea na maandalizi ya ujenzi wa madaraja 13 yakiendelea. Amesema utekelezaji wa miradi hiyo umefungua maeneo mbalimbali ya kiuchumi na kuongeza ufanisi wa sekta nyingine za usafiri ikiwemo reli, bandari na viwanja vya ndege.
Ulega amesema barabara zinaendelea kuwa mhimili mkuu wa usafiri nchini kutokana na kufika katika maeneo mengi zaidi ikilinganishwa na miundombinu mingine ya usafiri na usafirishaji.
Aidha, amesema Serikali inaendelea kulinda uwekezaji mkubwa uliofanywa katika miundombinu hiyo kwa kufanya matengenezo ya mara kwa mara. Katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, Serikali imefanya matengenezo ya kawaida ya barabara zenye urefu wa kilometa 16,782.58, matengenezo ya muda maalum kwa kilometa 1,101.12 pamoja na matengenezo ya sehemu korofi kwa kilometa 147.13 na madaraja 1,383.
Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha miundombinu ya barabara na madaraja inadumu kwa muda mrefu na kuwa salama kwa watumiaji wakati wote.

