Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wa Tanzania, Dkt. Leonard Akwilapo akisoma tamko la serikali ya Tanzania wakati akihutubia Mkutano wa Mawaziri kuhusu Ajenda Mpya ya Miji uliofanyika katika Kongamano la 13 la Miji Duniani (WUF13) mjini Baku nchini Azerbaijan leo tarehe 17 Mei 2026.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wa Tanzania, Dkt. Leonard Akwilapo (Kushoto) na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Prof Riziki Shemdoe wakiwa katika Mkutano wa Mawaziri kuhusu Ajenda Mpya ya Miji uliofanyika katika Kongamano la 13 la Miji Duniani (WUF13) mjini Baku nchini Azerbaijan leo tarehe 17 Mei 2026.

Na Mwandishi Wetu

Serikali ya Tanzania imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kutekeleza Ajenda Mpya ya Miji (New Urban Agenda – NUA) pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) kwa kuimarisha mipango ya Uendelezaji wa miji, huduma za msingi, uboreshaji wa miundombinu na makazi salama kwa wananchi.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 17 Mei 2026 na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wa Tanzania, Dkt. Leonard Akwilapo, wakati akihutubia Mkutano wa Mawaziri kuhusu Ajenda Mpya ya Miji uliofanyika katika Kongamano la 13 la Miji Duniani (WUF13) mjini Baku nchini Azerbaijan.

Katika hotuba yake, Dkt. Akwilapo alisema Tanzania inaunga mkono kaulimbiu ya WUF13 inayosema “Housing the World: Safe and Resilient Cities and Communities” akieleza kuwa kaulimbiu hiyo inaendana na malengo ya Maendeleo Endelevu SDGs hususani lengo la 11 pamoja na Ajenda Mpya ya Miji inayolenga kujenga miji salama, jumuishi, himilivu na endelevu.

Alisema karibu miaka 10 tangu kupitishwa kwa Ajenda Mpya ya Miji mwaka 2016 katika mkutano wa Habitat III mjini Quito, Ecuador, bado dunia inakabiliwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa makazi ya gharama nafuu pamoja na ukuaji wa makazi holela.

“Makazi bado ni gharama kwa watu wengi katika nchi zinazoendelea na hata zilizoendelea huku dunia ikiwa nyuma katika kufikia lengo la kuwa na miji salama, himilivu na endelevu kama ilivyoainishwa katika SDG 11,” alisema.

Alieleza kuwa, Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea na utekelezaji wa SDGs na Ajenda Mpya ya Miji katika mipango yake ya maendeleo ya taifa pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Waziri Akwilapo alisema Tanzania imepiga hatua katika maendeleo ya miundombinu, huduma za maji, nishati, afya na elimu sambamba na kuendelea kuboresha huduma za kijamii kwa wananchi.

Kuhusu makazi holela, alisema serikali imebadili sera kutoka ubomoaji wa makazi kwenda uboreshaji wa makazi hayo kwa kushirikisha wananchi pamoja na kurasimisha umiliki wa ardhi ili kuboresha maisha ya wakazi wa maeneo hayo.

“Serikali imeendelea kuimarisha upangaji matumizi ya ardhi, kuboresha huduma za msingi pamoja na kuhalalisha umiliki wa ardhi kwa lengo la kujenga miji endelevu na himilivu,” alisema.

Hata hivyo, Dkt. Akwilapo alikiri kuwa Tanzania kama zilivyo nchi nyingine zinazoendelea bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali katika utekelezaji wa Ajenda Mpya ya Miji ikiwemo ongezeko kubwa la watu mijini, uhaba wa rasilimali fedha na upungufu wa wataalam katika sekta.

Alisema pamoja na changamoto hizo, Tanzania ina matumaini kuwa kupitia mifumo jumuishi ya taasisi na ushirikiano madhubuti, lengo la kuhakikisha hakuna mtu anayeachwa nyuma litafikiwa.