Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Wizara ya Fedha, Bw. Lusius Mwenda, akimshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, kwa uamuzi wa kutoa huduma za uchunguzi wa viashiria vya magonjwa ya moyo pamoja na elimu kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kwa Watumishi wa Wizara ya Fedha, katika ukumbi wa Kambarage, jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Wizara ya Fedha, Bw. Lusius Mwenda (kulia), wakati wa zoezi la kutoa elimu kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kwa Watumishi wa Wizara ya Fedha, katika ukumbi wa Kambarage, jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, akieleza kuhusu madhara ya kunywa pombe kupita kiasi na matumizi makubwa ya sukari kama miongoni mwa visababishi vya magonjwa ya moyo, wakati wa zoezi la utoaji elimu kwa Watumishi wa Wizara ya Fedha, katika ukumbi wa Kambarage, jijini Dodoma.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bi. Scola Malinga (kulia) akiagana na Mtaalamu wa Maabara kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), baada ya kupata vipimo vya viashiria vya magonjwa ya moyo, katika ukumbi wa Kambarage, Wizara ya Fedha, jijini Dodoma.

Baadhi ya viongozi wa Idara, Vitengo na Watumishi wa Wizara ya Fedha, wakipata huduma za vipimo vya viashiria vya magonjwa ya moyo, katika ukumbi wa Kambarage, Wizara ya Fedha, jijini Dodoma.

Baadhi ya viongozi wa Idara, Vitengo na Watumishi wa Wizara ya Fedha, wakisikiliza maelezo ya Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge kuhusu viashiria vya magonjwa ya moyo, katika ukumbi wa Kambarage, Wizara ya Fedha, jijini Dodoma.

Watumishi wa Wizara ya Fedha wakipata huduma za vipimo vya viashiria vya magonjwa yasiyoambukiza, katika ukumbi wa Kambarage, Wizara ya Fedha, jijini Dodoma.

Watumishi wa Wizara ya Fedha wakipata elimu ya magonjwa yasiyoambukiza, katika ukumbi wa Kambarage, Wizara ya Fedha, jijini Dodoma. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha)
…..
Na. Peter Haule, WF, Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, amewataka Watumishi wa Wizara ya Fedha na wananchi kwa ujumla kuwa makini na taarifa zisizo sahihi kuhusu lishe kupitia mitandao ya kijamii, ikiwemo taarifa zinazopinga matumizi ya vyakula vya wanga kwa watoto.
Rai hiyo imetolewa katika Ukumbi wa Kambarage, Wizara ya Fedha jijini Dodoma, wakati wa zoezi la utoaji wa huduma za uchunguzi wa viashiria vya magonjwa ya moyo pamoja na elimu kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza, ikiwemo magonjwa ya moyo, kwa watumishi wa Wizara ya Fedha.
Dkt. Kisenge alisema kuwa utoaji wa elimu kuhusu matumizi ya vyakula vya wanga inapaswa kuzingatia umri na hali ya afya ya mtu, kwani watoto na vijana wengi bado wanahitaji wanga kwa maendeleo yao ya mwili na akili, hususan wale wasiokuwa na changamoto za kiafya.
“Vijana na watoto wanahitaji vyakula vya wanga kwa ajili ya kupata nguvu na kusaidia ukuaji wa akili, upungufu wa wanga unaweza kusababisha watoto kuwa na uwezo mdogo wa kufikiri na kujifunza”, alisema Dkt. Kisenge.
Alisisitiza kuwa jambo muhimu ni kuhakikisha watoto wanapata lishe kamili kwa ajili ya ukuaji wao.
Alisema kuwa mahitaji ya vyakula hubadilika kulingana na umri, akibainisha kuwa watu wenye umri wa zaidi ya miaka 50 wana vihatarishi zaidi vya magonjwa yasiyoambukiza ikilinganishwa na vijana.
Aidha Dkt. Kisenge, alitoa wito kwa Watumishi wa Wizara ya Fedha na watanzania kwa ujumla kula mlo kamili hususani vyakula vya asili zikiwemo mbogamboga na matunda ili kulinda afya za miili yao.
Akieleza kuhusu matumizi ya chumvi alisema kuwa wapo wanaopinga matumizi ya chumvi, alisema chumvi ni muhimu kwa maisha ya binadamu ikitumiwa kwa usahihi.
Vile vile amewataka Watumishi wa Wizara ya Fedha kuepuka matumizi ya yaliyopita kiasi ya pombe, vinywaji vinavyoongeza nguvu na kufanya kazi kupita kiasi, ametoa wito wa kupata mlo kamili, kufanya mazoezi na kuwa na utamaduni wa kupima afya.
Alisema kuwa utamaduni wa kupima afya unasaidia kupunguza gharama kubwa za matibabu na pia kumfanya mtumishi kuendelea kutoa huduma kwa wananchi kwa ufanisi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Wizara ya Fedha, Bw. Lusius Mwenda, alisema kuwa ili Wizara ya Fedha iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi unaotarajiwa, ni muhimu watumishi kuwa na afya njema.
Alisema ukosefu wa elimu kuhusu masuala ya afya unaweza kusababisha kupuuzwa kwa viashiria muhimu vya magonjwa vinavyohitaji kufanyiwa kazi mapema.
Bw. Mwenda aliishukuru JKCI kwa kutoa huduma hizo muhimu pamoja na ahadi ya kuendelea kufanya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali kila mwaka kwa watumishi wa Wizara ya Fedha.
Aidha, alisema watumishi wameonesha mwitikio mkubwa kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi hilo ili kupata elimu ya afya na huduma za uchunguzi kutokana na umuhimu wake.
Alibainisha kuwa watumishi wa Wizara ya Fedha watatumia vizuri elimu waliyoipata kuhusu mtindo bora wa maisha, lishe sahihi na umuhimu wa kufanya mazoezi, ili kuwa na afya njema itakayosaidia kutoa huduma kwa watanzania kwa ufanisi.
