Wajadili Kilimo himilivu na uendelezaji wa Kilimo Biashara

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 11, 2026 amekutana na Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Alvaro Lario, jijini Nairobi, Kenya, ambapo wamejadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano katika sekta ya kilimo na uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na IFAD katika maeneo mbalimbali ikiwemo kilimo himilivu cha tabianchi, maendeleo ya kilimo biashara, mapinduzi ya kidijitali katika sekta ya kilimo pamoja na uwezeshaji wa vijana na wanawake kiuchumi.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Tanzania inatarajia kuendelea kushirikiana na IFAD katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ya kilimo ikiwemo mpango wa kuongeza uzalishaji wa alizeti ili kusaidia kuongeza upatikanaji wa mafuta ya kula nchini.

“Kimekuwa ni kikao kizuri kwa sababu tumekuwa na ushirikiano nao kwa muda mrefu, ambapo katika kipindi kilichopita tumeshirikiana nao katika miradi mbalimbali, na hasa miradi katika sekta za uzalishaji”.

“Lakini pia tumedhamiria kuendelea kushirikiana katika kuendeleza mazao ya mchanganyiko ambayo katika miaka ya nyuma ilikuwa inachukuliwa kuwa ni mazao ya chakula peke yake, kwasasa mazao haya niya biashara na tunayafanya sehemu ya kukuza biashara ambayo Tanzania inafanya na nchi nyingine”

Ameongeza kuwa Tanzania inatarajia kuendelea kushirikiana na IFAD katika sekta ya mifugo na mazao ya baharini kwa upande wa Zanzibar.

“Sambamba na hayo, tunategemea kushirikiana nao katika utekelezaji wa kilimo endelevu ambacho kinasaidia kampeni yetu ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi nchi”. Amesisitiza Dkt. Mwigulu

Kwa upande wa Rais wa IFAD Alvaro Lario, amesema kuwa wataendelea kuhakikisha mipango na utekelezaji wa IFAD vinaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Tanzania 2050

“Kwasasa tunasubiri kusikia vipaumbele ya Tanzania ili tujue namna gani tunaweza kusaidia katika maeneo vya utoshelevu na usalama wa chakula pamoja na uongezaji thamani wa mazao”