*Makambako, Njombe.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, amewataka wananchi wa Wilaya ya Makambako mkoani Njombe na Watanzania kwa ujumla kuilinda na kuithamini miradi ya Umwagiliaji inayotekelezwa na Serikali kwa kuwa ni mali yao iliyolenga kuwakwamua kiuchumi.
Akizungumza na wananchi Wilayani Makambako, Waziri Mkuu Mwigulu , amebainisha kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya mapinduzi makubwa kwa kubadilisha mfumo wa kilimo kutoka kutegemea mvua pekee na kuelekeza nguvu kwenye sekta ya Umwagiliaji nchi nzima.
Mhe. Waziri Mkuu ameeleza kuwa Serikali imefanya maboresho makubwa ambapo miradi ya Umwagiliaji imeongezeka kutoka miradi 13 iliyokuwepo awali hadi kufikia miradi 780 inayotekelezwa hivi sasa.
Aidha, ameongeza kuwa eneo la kilimo cha Umwagiliaji limepanuliwa kutoka hekta 560,000 hadi kufikia hekta 980,000, huku lengo likiwa ni kuvuka hekta milioni moja hivi karibuni.
Alisisitiza kuwa bajeti ya sekta ya kilimo pia imepata msukumo mkubwa ikipanda kutoka shilingi bilioni 294 hadi kufikia shilingi trilioni 1.1, ikiwa ni ongezeko la zaidi ya mara tano.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Bw. Raymond Mndolwa, ameeleza kuwa katika eneo hilo la Makambako, Serikali inaenda kuwekeza zaidi ya shilingi bilioni 30 katika mradi mkubwa wa Umwagiliaji katika eneo la Idofi Wilayani Makambako.
Amesema, mradi huo utahusisha upanuzi wa eneo la kilimo kutoka hekta 300 zilizokuwa zikitumiwa na wananchi hadi kufikia hekta 1,300, jambo ambalo litaongeza tija na uzalishaji.
Vilevile, Bw. Mndolwa amebainisha kuwa mradi huo utajumuisha ujenzi wa stendi ya magari, soko la kisasa, na miundombinu ya kuhifadhia mbogamboga ili kusaidia wananchi kupata soko na kuzuia upotevu wa mazao baada ya kuvuna.
Aidha Mndolwa amesema kuwa mkandarasi ameshapatikana na mkataba wa kuanza wa kazi hiyo unatarajiwa kusainiwa wiki ijayo ili utekelezaji wake uanze mara moja kwa faida ya wananchi wa Makambako.

