Na John Bukuku, Dar es Salaam
Machi 4, 2026 – Mpango wa Wazo Bora Pitch umehitimishwa kwa mafanikio kwa kutoa jumla ya Sh milioni 17 kama mtaji wa kuanzisha na kukuza biashara kwa wajasiriamali waliobobea, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa RISE/E unaofadhiliwa na Standard Chartered Foundation.
Hatua hiyo imekuja kufuatia tangazo la hivi karibuni kwamba Standard Chartered Bank Tanzania ilitoa mchango wa Dola za Marekani 11,500 kwa Challenges Worldwide Tanzania ili kuchochea ukuaji wa ujasiriamali nchini.
Wazo Bora Pitch ni kilele cha programu ya mafunzo ya kina iliyofadhiliwa kupitia msaada wa Benki hiyo na kutekelezwa na Challenges Worldwide Tanzania. Mpango huo ulianza Desemba 2025 kwa tangazo la mwezi mmoja la kupokea maombi, lililovutia idadi kubwa ya wajasiriamali kutoka sekta mbalimbali.
Baada ya kufungwa kwa dirisha la maombi, washiriki 15 walichaguliwa kushiriki katika mafunzo maalum (bootcamp) yaliyolenga kuboresha mifumo ya biashara, kuimarisha usimamizi wa fedha na kuongeza utayari wa kupokea uwekezaji. Kati yao, washiriki saba waliingia hatua ya mwisho ya mashindano ya uwasilishaji wa mawazo (pitch) yaliyofanyika wiki hii jijini Dar es Salaam.
Katika matokeo ya mashindano hayo, Ng’oga Masheri Kaswahili alitangazwa mshindi na kujinyakulia Sh milioni 10 kama mtaji wa kuanzisha au kukuza biashara yake. Nafasi ya pili ilichukuliwa na Mohamed Muhidini aliyepokea Sh milioni 4, huku Nipaeii Mtana akishika nafasi ya tatu na kutunukiwa Sh milioni 3.
Jumla ya Sh milioni 17 zilizotolewa zinatarajiwa kusaidia upanuzi wa biashara, uundaji wa ajira na kukuza masoko kwa washindi hao.
Wazo Bora Pitch ni sehemu ya mpango mpana wa RISE/E ulioanzishwa mwaka 2024 kupitia Standard Chartered Foundation. Mpango huo wa miaka mitatu wenye thamani ya Sh bilioni 2.2 unalenga kusaidia moja kwa moja biashara ndogo 340 na kuunda ajira mpya 478 kote nchini, ukiweka mkazo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
Akizungumza kuhusu mafanikio ya mpango huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Standard Chartered Bank Tanzania, George Binde, alisema benki hiyo inajivunia kuona matokeo ya uwekezaji wake yakionekana wazi kupitia ukuaji wa washiriki na uimara wa mawazo yao ya biashara.
Alisema mtaji huo wa kuanzisha biashara utasaidia kubadilisha fursa zilizopo kuwa mafanikio yanayopimika na kuchangia katika kukuza uchumi shirikishi.
Hitimisho la Wazo Bora Pitch linaimarisha dhamira ya pamoja ya Standard Chartered Bank Tanzania na Challenges Worldwide Tanzania ya kuwawezesha wajasiriamali kujenga biashara imara zinazozalisha ajira na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.





