Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Mhe. CP. Suzan S. Kaganda, amekutana na kuzungumza na Balozi wa China nchini humo, Mhe. Zhou Ding, ambapo wamejadili masuala muhimu yanayolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na China.
Katika mazungumzo hayo, Balozi Kaganda ameishukuru Serikali ya China kwa kuendelea kuwa mshirika mkubwa wa maendeleo wa Tanzania, hususan kupitia ufadhili na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa madaraja, barabara na reli za kisasa. Amesema miradi hiyo imekuwa na mchango mkubwa katika kukuza uchumi na kuimarisha huduma kwa wananchi.
Aidha, Mhe. Kaganda ameeleza kuwa China imeendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta ya elimu kupitia utoaji wa ufadhili wa masomo kwa vijana wa Kitanzania katika ngazi na taaluma mbalimbali. Amesisitiza kuwa ushirikiano huo ni uthibitisho wa dhamira ya China kuendeleza sio tu Serikali ya Tanzania, bali pia maendeleo ya mwananchi mmoja mmoja.
Kwa upande wake, Balozi Zhou Ding amemshukuru Mhe. Kaganda kwa kufanya ziara hiyo ya kikazi na kusisitiza kuwa China itaendelea kudumisha na kuimarisha ushirikiano wake wa muda mrefu na Tanzania. Amesema uhusiano huo umejengwa juu ya misingi ya kihistoria, ikiwa ni pamoja na ushirikiano uliokuwapo tangu enzi za utekelezaji wa Sera ya Ujamaa chini ya waasisi wa mataifa hayo mawili.
Aidha, Balozi Ding amebainisha kuwa Zimbabwe ni miongoni mwa nchi za Afrika ambazo zimefaidika na urafiki wa Tanzania na China, akifafanua kuwa mchango wa Tanzania katika harakati za ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika, ikiwemo Zimbabwe, umeendelea kuheshimiwa na kuthaminiwa.




