Upo ushahidi madhubuti unaoonesha uwepo wa tija ya kupiga kura Katika uchaguzi Mkuu wa Tanzania licha ya uwepo wa mitazamo na kauli mbalimbali kuwa kushiriki kwenye uchaguzi huo ni kupoteza muda tofauti na uhalisia ulivyo, uchaguzi ukitajwa kama heshima, wajibu na silaha ya Kidemokrasia kote duniani.
“Kupiga kura ni haki ya Kikatiba, inayomuwezesha kila Mtanzania kushiriki katika maamuzi ya nchi kwa njia ya amani, kupitia kura wananchi huamua ni nani awaongoze katika nafasi za kisiasa kama Rais, Wabunge na Madiwani na hii ni njia halali ya kushiriki katika ujenzi wa Taifa na kuhakikisha kuwa sauti ya mwananchi inasikika.” Amesema Mchambuzi wa siasa Ally Said alipozungumza nasi.
Kulingana na Mchambuzi huyo, wananchi wanapojitokeza kwa wingi kupiga kura wana nafasi ya kuchagua Viongozi waadilifu na wenye uwezo wa kuwaletea maendeleo, kupitia kura matatizo ya huduma duni za jamii yanaweza kushughulikiwa, Kura ikiimarisha pia misingi ya demokrasia na utawala bora kwa kuwafanya walioko madarakani kuwajibika kwa wananchi kwa kujua kuwa wanaweza kuondolewa kwa kura ikiwa hawatatimiza wajibu na ahadi zao.
John James, Mwananchi wa Goba Jijini Dar Es salaam anasema anafahamu kuhusu haki yake ya kupiga kura, akihimiza umuhimu wa kuwachagua wale wanaojua shida za wananchi na wenye kujali mahitaji ya wananchi. Akieleza kuwa mabadiliko ha kweli yanapatikana kupitia kura na si vurugu, matusi, jazba ama maandamano ya kutaka kushinikiza mambo isivyo halali.
Ushiriki wa uchaguzi unatoa nafasi kwa wananchi kushiriki moja kwa moja katika maamuzi yanayogusa maisha yao ya kila siku ambapo Viongozi wanaochaguljwa kwa ushirikishwaji wa wananchi wanakuwa na uwezo wa kutengeneza mipango ya maendeleo inayokidhi mahitaji halisi ya eneo husika, wito ukitolewa kwa kila mwananchi mwenye sifa kujitokeza kupiga kura kwa amani, kuheshimu sheria za nchi ikiwa ni pamoja na kuepuka kuvunja sheria kwa kuhamasisha wananchi kutokupiga kura ama kulinda kura kwenye Vituo vya upigaji kura.