Muogeleaji Singko Steiner wa Taliss-IST akishindana
………………………………………………………………………………..
Na Mwandishi Wetu
Dar es Salaam. Jumla ya klabu tisa zitashiriki katika mashindano ya kuogelea ya Taliss-IST yaliyopangwa kufanyika Jumamosi na Jumapili kwenye bwawa la kuogelea la Shule ya Kimataifa ya Tanganyika (IST-Masaki) jijini.
Klabu hizo zitatoa jumla ya waogeleaji 228 ambao watashindana katika staili tano pamoja na relai kwa mujibu wa Meneja wa taliss-IST- Hadija Shebe.
Hadija alizitaja klabu hizo na ida ya waogeleaji wake kwenye mabano kuwa ni Bluefins itawakilishwa na waogeleaji 39 na klabu ya Dar es Salaam Swimming Club (DSC) itawakilishwa na waogeleaji 31 na Wahuu ya Zanzibar ambayo itawakilishwa na waogeleaji sita.
Alizitaja klabu nyingine kuwa ni Shule ya Kimataifa ya Morogoro (Mis Piranhas ) ambayo itakuwa na waogeleaji 27 wakati klabu mpya ambayo inakuja kwa kasi, FK Blue Marlins itawakilishwa na waogeleaji 25, UWCEA (13) na waogeleaji tisa wataiwakilisha klabu ya Braeburn.
Alisema kuwa jumla ya staili tano zitashindaniwa na waogeleaji katika mashindano hayo yaliyodhaminiwa na Jubilee Insurance na Nissan ambao ni wadhamini wakuu, Burger 53, Subway, FLM Catering na Azam. Staili hizo ni free, butterfly, backstroke, breaststroke na Individual Medley.
Waogeleaji watashindana katika umri tofauti ambao ni chini ya miaka nane, miaka tisa na 10, miaka 11 na 12, 13 na 14 na kuanzia miaka 15 na kuendelea. Alisema pia kutakuwa na mashindano ya wazi ambayo yatashirikisha waogeaji wenye umri tofauti.
“Kutakuwa na jumla ya mashindano 105 ambapo siku ya kwanza, waogeleaji watashindana katika mashindano 71 na siku ya pili watamzalizia. Washindi katika kila umri watazawadiwa vikombe na washindi katika kila tukio watazawadiwa medali mbalimbali,” alisema.