Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu akishiriki maadhimisho ya Siku ya Mashujaa katika uwanja wa Mashujaa, Mtumba Jijini Dodoma leo, tarehe 25 Julai, 2025.
………..
RAIS NA AMIRI JESHI MKUU SAMIA ASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA KUMBUKUMBU YA MASHUJAA
Na Meleka Kulwa – Dodoma
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo ameongoza maelfu ya wananchi pamoja na viongozi mbalimbali wa kitaifa katika maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa yaliyofanyika katika Uwanja wa Mnara wa Mashujaa, uliopo katika Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.
Maadhimisho hayo ni sehemu ya heshima za kitaifa kwa mashujaa waliopigania uhuru na kulinda mipaka ya Tanzania tangu enzi za harakati za ukombozi hadi sasa.
Rais Samia aliambatana na viongozi wa juu wa serikali akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi pamoja na Makamu wa Rais, Naibu Mkuu na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Katika tukio hilo la kihistoria, Rais Samia aliweka mkuki na ngao katika Mnara wa Mashujaa kama ishara ya kuenzi na kuthamini mchango wa mashujaa waliolitumikia taifa kwa ujasiri na kujitolea.
Aidha, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Brigedia Jenerali John Mkunda naye aliweka sime katika mnara huo, huku gwaride rasmi likipamba maadhimisho hayo kwa heshima ya mashujaa wote waliotangulia mbele ya haki
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye Maadhimisho ya siku ya kumbukumbu ya Mashujaa katika uwanja wa Mashujaa Mtumba Jijini Dodoma tarehe 25 Julai, 2025.