Na Ashrack Miraji Fullshangwe Media
Mkuu wa Wilaya ya Same Mheshimiwa Kasilda Mgeni ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Same kwa kutoa mkopo wa asilimia 10 za mapato ya ndani kwa wakati ili kuwainua wananchi kiuchumi.
Pongezi hizo zimetolewa na Mkuu wa Wilaya wakati akikabidhi hundi ya Shilingi Milioni 210 ambazo ni Mkopo wa robo ya nne kwa wanawake ,Vijana na watu wenye ulemavu.
“Nimpongeze Sana Mkurugenzi kwa kuhakikisha kuwa Mkopo huu unatolewa kwa wakati”alisema Mheshimiwa Kasilda
Akizungumza kwenye hafla hiyo Mkurugenzi Mtendaji WA Halmashauri ya Wilaya ya Same Bw.Jimson Mhagama amewataka wanufaika wa mkopo kuhakikisha kuwa wanarejesha fedha hizo kwa wakati.
“Serikali imewaamini hivyo hamna budi kuimarisha imani yenu kwa Serikali kwa kurejesha kwa wakati”amesema Mhagama
Kwa upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii Wilaya ya Same Bw.Anatoly Charles amesema jumla ya vikundi 36 vimenufaika na Mkopo huo ambapo vikundi 24 ni vya wanawake,Vijana ni vikundi 9 na watu watatu wenye ulemavu.
Amesema kwa mwaka wa fedha 2024/2025 Halmashauri ya Wilaya ya Same imetoa Mkopo wa Shilingi Milioni 585.5 kwa vikundi 113.