Baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam wamepongeza kazi na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, wakisema kuwa zimekuwa na mchango mkubwa katika kuhakikisha haki, utawala bora, na usimamizi wa sheria nchini.
Hayo yamesemwa na wananchi hao tarehe 23 Juni, 2025 walipotembelea banda la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (MSLAC) inayoendelea Jijini Dar es Salaam.
Akizungumza baada ya kupata huduma katika banda la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali mmoja wa Wananchi Bi. Sharifa Mohamed ameipongeza ofisi hiyo kwa kuboresha upatikanaji wa Msaada wa Kisheria, kutoa Elimu ya Sheria kwa umma, na Kushughulikia Changamoto mbalimbali za Kisheria zinazowakabili wananchi.
“Kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, wananchi wa kawaida kama sisi sasa tunaelewa haki zetu. Elimu ya Sheria kwa jamii imeongezeka, na tunaona matokeo yake katika namna haki inavyotendeka.” Amesema Bi. Sharifa.
Kwa upande wake, Bw.Abdalah Sonda amefurahishwa na huduma aliyoipata kutoka kwa Mawakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambapo changamoto yake kuhusu ardhi iliyokuwa inamsumbua kwa muda mrefu imepatiwa ufumbuzi.
“Nimefika hapa nimepokelewa vizuri na kupata ushauri mzuri nilikuwa na tatizo la ardhi nimehangaika nalo kwa miaka nane ila baada ya kuja hapa nimeelekezwa na sasa naona linaenda kutamatika ninawashukuru sana”.
Naye, Bw. Khalid Luswaga amesema kuwa kutoka na jitihada zinazofanywa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika kuelimisha wananchi masuala ya kisheria kumeongeza uelewa kwa Wananchi wa kufahamu haki zao na maboresho mbalimbali ya sheria yameongeza uwazi na uwajibikaji katika sekta mbalimbali.
“Huduma zinazotolewa ni nzuri na zinawasaidia sana wananchi kuelewa namna ya kudai na kupata haki zao nawaomba elimu hii iwe endelevu.” Amesema Bw. Khalid
Kwa upande wake, Wakili wa Serikali Mkuu Bi. Violeth Eseko ameridhishwa na mwitikio wa wananchi kutembelea banda la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali huku akitaja masuala ya Ardhi, Ajira, Ndoa na Matunzo ya Watoto ni miongoni mwa changamoto zilizoletwa na wananchi, ambapo baadhi zimeshughulikiwa hapohapo na baadhi zimechukuliwa kwa ajili ya kupata ufumbuzi zaidi.
“Wananchi wamejitokeza kwa wingi, wengi wao wamekuwa na changamoto za kisheria zinazohusu Ardhi, Ndoa, Ajira na Matunzo ya Watoto, zipo ambazo tumezishughulikia na kuzimaliza hapahapa na nyingine tumezichukua kwa hatua zaidi.”
Aidha Bi. Violeth ametoa wito kwa Wananchi kuendelea kutembelea banda la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu katika Kampeni hiyo ili waweze kupata huduma za Ushauri wa Kisheria, Elimu ya Sheria, na Utatuzi wa Malalamiko mbalimbali.
Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (MSLAC) kwa Jiji la Dar es Salaam ilianza tarehe 16 Juni, 2025 na itaendelea hadi tarehe 25 Juni, 2025 kwa wananchi kupata huduma mbalimbali za Kisheria bila malipo.