Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) amewasili Beijing, China tarehe 9 Juni, 2025 kwa ziara ya kikazi na kupokelewa na Kiongozi wa Ngazi ya Juu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri wa Watu wa China, Bw. Xu Zhongsheng pamoja na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini China, Mhe. Khamis Mussa Omar.
Akiwa nchini China, Mheshimiwa Waziri Kombo ataongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Mawaziri wa kufuatilia utekelezaji wa maazimio ya Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (Forum on China-Africa Cooperation-FOCAC Coordinators Meeting) utakaofanyika kuanzia tarehe 11 hadi 12 Juni 2025 na maonesho ya nne (4) ya kimataifa ya biashara kati ya China na Afrika yatakayofanyika tarehe 13 hadi 15 Juni, 2025 katika jiji la Changsha.
Aidha, pembezoni mwa mkutano huo Waziri Kombo atafanya mazungumzo na Mheshimiwa Wang Yi, Mjumbe wa Ofisi ya Siasa ya Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China (CCP) na Waziri wa Mambo ya Nje wa China kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kimkakati kati ya Tanzania na China.
Vilevile, Waziri Kombo na ujumbe wake watatembelea majimbo ya Sichuan na Shenzhen, ambapo watakutana na viongozi wa mikoa hiyo pamoja na kampuni mashuhuri za biashara na uwekezaji za China. Mikutano hiyo inalenga kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na China, hasa katika masuala ya kisiasa na kiuchumi na kuhamasisha kampuni za China kuja kuwekeza nchini.
Pamoja na masuala mengine Waziri Kombo atatembelea Ofisi ya Ubalozi Mdogo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mjini Guangzhou na kukutana na Watanzania waishio katika jiji hilo.