Na. Anangisye Mwateba- Bungeni Dodoma
Wizara ya Maliasili na Utalii katika kipindi cha mwaka 2024/2025 imebaini vivutio vipya vya utalii 337 katika Mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma, Iringa, Njombe, Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi na Kigoma.
Haya yamebainishwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dunstan Kitandula (Mb) alipokuwa akijibu swali na Mhe. Prof. Patrick Alois Ndakidemi aliyetaka Kujua Serikali ina mkakati gani wa kupanua wigo wa maeneo mapya ya utalii nchini.
Mhe. Kitandula aliongeza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na utalii imekuwa ikitekeleza mikakati mbalimbali inayolenga kupanua wigo wa mazao ya utalii nchini ili kuvutia watalii wengi zaidi, kuongeza siku za watalii kukaa nchini, kuongeza mapato yatokanayo na shughuli za utalii pamoja na kupunguza utegemezi katika zao la utalii wa wanyamapori nchini.
Vilevile Mhe. Kitandula alisema kuwa serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutoka sekta za umma na binafsi kuendeleza mazao ya utalii ya kimkakati ikiwemo utalii wa fukwe, meli, mikutano na matukio, malikale, utamaduni na michezo.
“katika kuendeleza utalii wa meli nchini, Serikali imekuwa ikishirikiana na wadau wa sekta binafsi wenye mtandao mkubwa katika soko la kimataifa la utalii wa meli kutangaza zao hili. Katika kipindi cha Julai, 2024 hadi Machi, 2025, jumla ya meli za kitalii 9 ziliwasili nchini na kuleta watalii 2,944 waliotembelea vivutio mbalimbali vya utalii” alisema Mhe. Kitandula