Baadhi ya Wafanyakazi Wanawake wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Temeke wakiwa katika utekelezaji wa majukumu ikiwemo kuboresha miundombinu ya umeme katika maeneo mbalimbali katika mkoa huo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya kuelekea kilele cha siku wanawake Duniani yatakayofanyika Kitaifa Machi 8, 2025 Mkoani Arusha (PICHA NA NOEL RUKANUGA)
…………
Wafanyakazi Wanawake wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Temeke wametekeleza majukumu kwa ufanisi mkubwa kwa kufanya kazi muhimu ikiwemo kutengeneza miundombinu ya umeme katika maeneo mbalimbali pamoja na kutoa huduma kwa wateja ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani yatakayofanyika Kitaifa Machi 8, 2025 Mkoani Arusha.
Wakizungumza kuhusu umuhimu wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Wafanyakazi hao, Wameushukuru uongozi wa TANESCO Mkoa wa Temeke kwa kutambua umuhimu wa Wanawake na kutoa fursa ya kutoa huduma kwa wateja katika nyanja mbalimbali katika wiki hii ya kuelekea kilele Cha siku ya Wanawake Duniani.
Fundi Kitengo Cha Matengezo TANESCO Mkoa wa Temeke Betha Sambo, amewahasa wanawake kutambua majukumu yao katika jamii inayowazunguka pamoja na kudumisha upendo na mshikamano, huku akisisitiza umuhimu wa kujiamia pamoja na kuwa na utamaduni wa kufanya kazi za ufundi kwani sio ngumi kama baadhi ya watu wanavyodhani.
“Wanawake tusiogope kujihusisha na shughuli za kiufundi, kwani sio ngumu cha muhimu ni kijitoa kwa moyo wote ili kufikia malengo” amesema Sambo.
Mhasibu Mkuu wa TANESCO Mkoa wa Temeke Lucy Mwaisemba, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwashika mkono wanawake katika nyanja mbalimbali pamoja na kufanya uwezeshaji ili kuhakikisha huduma ya nishati ya umeme inapatikana ya uhakika kwa wananchi.
Nea, Afisa Ugavi TANESCO Mkoa wa Temeke, Enatha Paul, amesema kuwa ni wajibu wao kuendelea kuwaelimisha wanawake wengine kuhusu umuhimu wa haki, usawa na uwezeshaji mahali pakazi, kujiamini, kuongeza juhudi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku kwa ajili ya ujenzi wa Taifa.
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka huu yamebeba kauli mbiu isemayo : “Wanawake na Wasichana 2025: Tuimarishe Haki, Usawa na Uwezeshaji.”
Kauli mbiu hiyo imelenga kuhimiza jitihada za kuleta usawa wa kijinsia, kuzingatia haki za wanawake na wasichana, na kuwapa uwezo wa kuchukua nafasi ya uongozi katika sekta mbalimbali.
Katika muktadha huu, wafanyakazi wanawake wa TANESCO Mkoa wa Temeke wanajivunia mchango wao katika sekta ya nishati, na wamesisitiza umuhimu wa kuendelea kutekeleza majukumu kwa ufanisi ili kuunga mkono malengo ya Taifa ya maendeleo endelevu.