*Mikakati kamambe ya kutanua wigo wa soko la Utalii yasukwa
Na Beatus Maganja
Kamisheni ya Utalii ya Zanzibar na Chama cha waongoza watalii Zanzibar (ZATO) Februari 06, 2025 walifanya ziara maalumu (Fam – Trip) katika Hifadhi ya urithi wa utamaduni wa dunia Magofu ya Kale Kilwa Kisiwani na Songo Mnara Mkoani Lindi ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kupanua wigo wa soko la utalii katika maeneo mbalimbali ya Tanzania Bara Kwa lengo la kukuza vivutio vya kihistoria na asili ili kuvutia watalii wengi zaidi.
Ziara hiyo iliyoratibiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania – TAWA inalenga kuimarisha ushirikiano kati ya Zanzibar na maeneo mengine ya bara yaliyo chini ya usimamizi wa TAWA na kuwawezesha wadau hao kuona vivutio vya utalii na fursa za uwekezaji pamoja na kujadili masuala ya kukuza na kutangaza utalii wa kimataifa.
Majadiliano na wadau hao wa Sekta ya utalii yaliwahusisha wawakilishi kutoka TAWA ambayo iliwakilishwa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi Kitengo cha Biashara Hamza Hassan, Mohammed Walid Fikirin kutoka Kamisheni ya utalii Zanzibar na Thabit Abdulrazak Abdulrahman wa ZATO.
Aidha majadiliano hayo yalijikita katika kusuka mikakati ya kutangaza vivutio vya Hifadhi ya Urithi wa Utamaduni wa Dunia Magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara, Pori la Akiba Pande na Hifadhi ya Magofu ya Kale Kunduchi pamoja na Pori la Akiba Wami-Mbiki Kwa lengo la kuvutia watalii kutoka pembe zote za dunia.
Hii ni sehemu ya jitihada zinazofanywa na Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii na TAWA kuunganisha Zanzibar na vivutio vya utalii vilivyopo mikoa ya Tanzania Bara ikiwa ni hatua muhimu katika kutangaza utalii wa kiutamaduni, kihistoria na wa asili huku zikiweka misingi ya kukuza uchumi wa Taifa Kwa njia endelevu.