Na Albano Midelo,Tunduru 

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Laban Thomas amezindua tawi jipya la Benki ya CRDB Tunduru hivyo kuwa ni tawi la 260 la benki hiyo nchini.

Akizungumza kabla ya kuzindua tawi hilo,Kanali Thomas  amesema kuzinduliwa kwa tawi hilo kunasogeza huduma za kibenki jirani na wananchi Pamoja na kufungua fursa za kuchumi kwa wajasirimali.

Amesisitiza kuwa uzinduzi wa tawi hilo utawawezesha wananchi kupata huduma zenye hadhi za kimataifa na kuisaidia jamii kupambana na umasikini.

“Fedha ni kichocheo muhimu cha maendeleo ya taifa lolote hivyo basi ukuaji wa sekta ya Benki ni muhimu sana katika kukuza Uchumi na kupunguza umaskini’’,alisisitiza RC Thomas.

Ameongeza kuwa sekta hiyo ina uwezo mkubwa wa kuwafikia na kuwahudumia wateja wengi wa mijini na vijijini ambapo amewaasa wananchi kutambua umuhimu wa kutumia huduma zao kwa maendeleo binafsi na Taifa kwa ujumla.

Ameiomba benki ya CRDB kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kutumia huduma za benki ili waweze kuweka akiba,kukopa na kurejesha mikopo kwa wakati.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Wateja Wadogo kutoka CRDB Makao makuu Boniventure Paulo akizungumza kabla ya uzinduzi huo amesema  CRBD inatoa mikopo ya  aina zote na kwamba benki hiyo ni kimbilio la wakulima.

Amesema hadi sasa Benki ya CRDB inaongoza  kwa kuwa na idadi kubwa ya wakulima ambao wamekopeshwa na kwamba wakulima wa Wilaya ya Tunduru watanufaika na Benki hiyo.

Amesisitiza kuwa wakulima na wateja wengine  kuweka akiba CRDB hali itakayosaidia usalama wa fedha zao ambapo amewatahadharisha wananchi kuacha kuweka fedha nyumbani na kusababisha upotevu kutokana na uvamizi wa majambazi au wezi  hivyo kuhatarisha usalama wa Maisha.

Amewashauri wafanyabiashara,wajasirimali, wafanyakazi na wananchi wengine kuzitumia fursa zilizopo wilayani Tunduru kukuza kipato chao ambapo amesisitiza uwezeshaji wa vijana na wanawake ni jambo ambalo litapewa kipaumbele kwenye benki hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Laban Thomas mwenye mkasi akikata utepe kuzindua tawi la 260 la CRDB wilayani Tunduru 

Baadhi ya wadau wakiwa kwenye uzinduzi wa tawi jipya la CRDB mjini Tunduru